Sijui wewe lakini hivi ndivyo nilivyoona mimi na katika kazi zangu mimi hiki ndiyo ninachokutana. Mwanaume anapowaza kuhusu ndoa moja kwa moja akili yake huwaza kuhusu kujitegemea. Atawaza kuhusu kuwa na kazi nzuri yenye kipato cha kumuwezesha kuhuduia familia yake tarajiwa, atawaza kuhusu kuwa na nyumba au hata chumba cha kupanga (kuondoka nyumbani kwao na kuwa na kwake), atawaza kuhusu kila kitu namna ya kuhudumia mke.
Lakini mwanamke anapowaza kuhusu ndoa, anawaza mwanaume ambaye atamtimizia mahitaji yake yote, ambaye atakua na nyumba au chumba (hakai kwa wazazi), ambaye ana kazi ya kumuingizia kipato na mambo mengine kama hayo. Ndiyo maana wanawake wengi wanapokua na wachumba wao ambao bado huishi kwa wazazi wao huwasumbua ili kuhama na kutafuta chumba na kama hawana kazi basi huwa na mashaka na ndoa yenyewe!
Nijambo la kawaida sana kukuta mwanamke anaolewa akiwa hana kazi ya kumuingizia kipato, tena wengine wengi sana hata kulazimika kuacha kazi ili aolewe lakini ni nadra sana kukuta mwanaume anaoa akiwa hana kazi. Ninadra kukuta mwanaume anaacha kazi ili aoe, ngumu sana na hata kumpata huyo mwanamke ambaye atavumilia mwanaume ambaye hana kazi itabidi ufanye kazi ya ziada. Hakuna mwanaume anategemewa kufanya kazi na kuhudumia familia ni wajibu wa kiasili!
NINI KINATOKEA HAPA? Kinachotokea hapa nikua mwanaume anapotaka kuoa huwekeza katika maisha yake binafsi, anakua na kila kitu chake hivyo hata kama akiachana na mwanamke anachopoteza tu ni mwanamke na si kingine. Kwamba mwanaume anapoishi na mwanamke kama mpenzi tuseme miaka mitatu, katika miaka mitatu hiyo atakua amewekeza vitu vingi kiuchumi hivyo hata akiachika anampoteza mwanamke tu na maisha yake hayabadiliki. Hapa amewekeza akijiandaa kuoa bila kujali anamuoa nani bado vitu vyake ataendelea kuwa navyo kila siku!
Mwanaume akiachika sana atatafuta mwanamke mwingine tu basi. Lakini mwanamke anapokua kwenye mapezi basi hawekezi kihisia tu bali kimalengo, yaani badala ya kujiwekea malengo ya kufanikiwa mwenyewe huweka malengo ya kufanikiwa na yule mwanaume. Wanawake wengi wanapokua na wanaume na kuwa nao muda mrefu wakawa wameahidiwa ndoa basi huanza kuona mafanikio ya mwanaume kamamafanikio yao wenyewe.
Utakuta hata kama mwanamke anafanya kazi lakini katika kufanya mambo ya maendeleo atakua akimhamasisha zaidi mpenzi wake kuliko yeye na huridhika mpenzi wake anapofanya yale mambo. Mfano utakuta anamshauri kununua kiwanja na hata kumuongezea kidogo, anamshauri kuacha pombe na kufungua biashara, anamshauri asinunue Gari na kuanza kujenga. Kama mwanamke hupenda zaidi na kama jamaa kashajitambulisha utakuta binti huchukua hata mkopo kumpa mwanaume.
Kwake mwanaume akifanikiwa na yeye hujiona kama amefanikiwa utakuta mwanamke anajisifu kabisa kwa mashoga zake “Tunajenga Mbagala… tumenunua Gari nyingine… ndiyo tunamalizia ili tukifunga ndoa tunahamia kwetu… anajenga hataki akae kwao… nyumba za kupanga hatutaziweza… hatubadilishi gari sasa hivi…” Ndiyo kiasilia mwanamke anayependwa huanza kujimiliki na kuhisi yeye ni sehemu ya mali za mwanaume hivyo kutamani hata kuchangia kuzitafuta.
Binti hujisahau zaidi kama anauhuru wa vile vitu vya mwanaume, kwa mfano kaambiwa simamia mafundi, anapewa ufunguo anaweza kwenda wakati wowote kwa mwanaume bila taarifa, anapewa Gari na kulitumia kama lake, katika biashara anaweza kwenda kukaa na hata kuuza. Basi hujisahau na kwakua anaamini kuwa ataolewa basi huona kila kitu kama chake! Hii humfanya kusahau kabisa kuwa hata yeye ana maisha yake na anaweza kufanya vitu kama anavyofanya yule mwanaume.
Sasa binti kama huyu anapoachika haishii kupoteza mwanaume tu, anakua amepoteza muda wake pia lakini haiishii hapo anaumia zaidi kwakua amepoteza nguvu yake ya kuwekeza kwakua tu alimuunga mkono mwanaume au alijiaminisha kuwa wameshapata kwa pamoja. Unaachwa pamoja na kuwa ulikua na kazi lakini huna hata kiwanja, hujanunua hata gari, huna chochote, si kwasababu mshahara ulikua mdogo hapana kwasababu kila kitu ulikua unampa au ulishajiaminisha unacho kwakua mwanaume anacho.
UFANYE NINI SASA? Kama uko kwenye mahusiano na mwanaume yeyote, hata kama unampenda kama Malaika, hata kama anakupenda na kukujali, hata kama kashajitambulisha kwenu hata kama mnaishi pamoja na mtoto mnaye unatakiwa kutambua kitu kimoja kuwa “SI MUME WAKO!” narudia “SI MUME WAKO!” Kwa maana hiyo mwanaume huyu kwanza anaweza kukaucha wakati wowote bila kuwa na sababu yoyote na wala usidhani atapata laana yoyote.
Lakini pili kila kitu anachokimiliki basi jua ni chakwake na wewe kama kiko kwa jina lake basi jua kuwa huna haki nacho hata kama umechangia yeye kukipata, hata kama umemshauri mpaka basi, hata kama wewe ndiyo ulikua unasimamia, hata kama wewe ndiyo ulimpa wazo hata kama wewe ndiyo uliloga akakipata au hata kama ulifungwa akakipata. Narudia najua unahisi hatakuacha na mimi nakuombea Mungu asikiache lakini ukweli nikuwa si chako.
Wewe ni sawa na mpangaji, mpangaji hata kama unapatana vipi na mwenye nyumba, hata kama anakuruhusu kupokea kodi katika ile nyumba, hata kama anakuambia usilipe kodi na hata ukiikarabati vipi nyumba yake kamwe haiwezi kugeuka kuwa yako hivyo usijipe moyo kuwa ukimuudhi hutahama au usidhani kwakua umemsaidia kujenga ukuta na kupaka rangi akikufukuza mtagawana hapana, akikuchoka unaondoka tena bila hata chochote.
Kwahiyo kama unataka usiumie sana unapoachika hembu wekeza kivyako, huo ushauri mzuri unaompa mpenzi wako hembu jipe na wewe, kama ni kujenga badala ya kuwekeza katika kumsimamia nyumba yake wekeza katika kujisimamia, badala ya kumshauri kuhusu biashara jishauri na fungua wewe. Unatumia muda mwingi kumtengeneza yeye kufanikiwa wakati wewe umejisahau na huna chohote akikuacha unabaki kama kakichaa flani kwakua huna maisha bila yeye.
Basi hata kama ni lazima, hata kama haiwezekani unaona kabisa mnapendana mnataka muwekeze kwa pamoja, hembu kuwa na akili kidogo tu na sema tuandike majina yetu wawili. Kwamba muwe kama mnafanya kwa pamoja na si yeye anafanya na wewe unamuunga mkono. Akikuambia inamaana huniamini nikaweka jina langu mwenyewe muulize inamaana huniamini ukaweka majina yetu wote. Acha kutengeneza manyanyaso kwa kutokua na chakwako, hembu anza kutengeneza maisha yako sasa.