NDOA YA MAUTI; SITAMANI KUFA LAKINI SITAKI KUISHI --- SEHEMU YA KWANZA

0

“Dada huyo ni mume wako kweli?” Aliniuliza kijana mmoja ambaye alikuwa pale dukani. Nilimuangalia kwa wasiwasi nikataka kudanganya niseme labda ni bosi wangu lakini nilikumbuka wakati ananitukana alisema “Najuta kuoa mwanamke mbinafsi kama wewe! Unawatesa sana ndugu zangu!” 



Nilitaka pia kutokumjibu kwani yalikuwa hayamuhusu lakini alikuwa amenunua vitu vingi na kwa muonekano wake angekuwa ni mteja wa kudumu.


“Ni mume wangu ndiyo” Nilimjibu kwa kifupi huku nikijifanya niko bize kumuandikia risiti, sikutaka aendelee kunichunguza. Aliniangalia kwa huruma huku akitingisha kichwa kusikitika.


“Wanawake mnavumilia mengi sana...” Aliongea kwa masikitiko huku akipokea risiti niliyokuwa nikimkabidhi. Tayari vijana wangu walishamaliza kupakia mizigo aliyokuwa amenunua kwenye gari aliyokuja nayo aina ya Toyota Double Cabin.


Aliwakabidhi hela ya kupakia kisha akaingia kwenye gari na kuondoka zake. Nilimuangalia wakati anaondoka huku nikimshukuru Mungu uwepo wake pale kwani nina uhakika kama asingekuwepo basi siku ile ningechezea makofi. Mume wangu aliona aibu kunipiga mbele ya mwanaume mwenzake tena akiwa hamfahamu


Siku yangu ilianza kuharibika asubuhi, wakati nimeenda kuchukua vifaranga nilimuacha wifi na mfanyakazi pale dukani, niliporudi sikumkuta wifi yangu na nilipomuuliza mfanyakazi aliniambia aliondoka pale tu nilipoondoka na kusema anaenda Kariakoo.


Sikuwaza sana kwani ilikuwa ni kawaida yake alikuwa akifanya kazi anavyojitakia. Nilikasirika pale alipokuja Mama John mteja wangu mkubwa, nilimuambia mfanyakazi wangu kumpa shilingi laki tatu nilizokuwa nimemuachia asubuhi wakati naondoka ili Mama John akija kama sijarudi ampe.


“Dada amezichukua, amesema kuna vitu anaenda kununua mjini..!” Alinijibu akimaanisha wifi yangu kazichukua zile pesa. Hasira zilinipanda kwani wakati ule sikuwa na hata shilingi mfukoni, hela zote nilinunulia mzigo na Mama John ni mteja wangu wa muda mrefu, ilinilazimu kukopa kwa jirani na kumkabidhi huku nikijifanya hakuna kitu kibaya kilichotokea.


Haikupita nusu saa wifi yangu alirejea, hata kabla sijamsemesha alitoa maronya ronya ya nguo aliyonunua huko mjini na kuanza kumuonesha mfanyakazi na wamama wengine. Nilijua alikuwa anafanya makusudi ili niongee hivyo nilimuangalia tu bila kusema chochote.


Sikutaka watu wajue nimekasirika hivyo alipomaliza na kuingia dukani bila kusema chochote nilitulia mpaka mfanyakazi alipotoka ndipo kistaarabu nilipomuuliza mbona amechukua pesa za mteja wakati akijua hatuna pesa, pesa yote tulienda kununulia mzigo, angalau hata ungeniambia nijue cha kufanya.


Aliniangalia kwa dharau kisha akasema. 

“Kwani pesa ni zakwako, hizi mali ni za Kaka yangu na yeye nilimuambia akaniambia nichukue..”

“Hata kama lakini ungeniambia na mimi…”

“Bibieee! Nikuambie wewe ili? Hizo zote unazopeleka kwenu unatuambia? Mfyuuuu! Au unafikiri hatujui?”


Alisonya kwa nguvu, nilinyamaza tu bila kusema chochote. Ukimya kidogo ulitawala, ni kama alitaka niongeee lakini sikunyanyua tena mdomo wangu, alianza kuongea maneno yake ya kashfa, kusema sema na kusengenya lakini sikujibu chochote. Kuona vile alichukua nguo zake na kuondoka bila hata kuaga.


Jioni sasa baada ya mume wangu kutoka kazini ndiyo akaja pale, kakunja ndita na mihasira yake akisema ninamnyanyasia ndugu zake. Alinitukana matusi ya nguoni mbele ya wafanyakazi na wateja, nilimsikiliza bila kumjibu kwani nilijua nikinyanyua tu mdomo ni kipigo.


Hilo nalo lilikuwa kosa kuwa nina kiburi simjibu, simuongeleshi nina dharau na mambo kama hayo. Hata hivyo sikuongea, nilibaki tu kimya mpaka akaona kama anajichora akaondoka.


*****


Maisha yetu hayakuwa hivyo, baada ndoa maisha yetu yalikuwa mazuri, wakati huo ndiyo nilikuwa nimemaliza kidato cha sita, sikufaulu vizuri hivyo nilibaki nyumbani kwa kama miezi sita ndipo nilipoolewa na mume wangu ambaye alikuwa ni mhasibu.


Erick alikuwa akiishi nyumbani kwao, kama mtoto wa kwanza alichukua jukumu la kulea familia yao baada ya Baba yake kufariki. Alikuwa akiishi yeye Mama yake na wadogo zake wanne wawili wakike na wawili wakiume.


Mwanzoni mambo yalikuwa mazuri kidogo, Mama mkwe na wifi zangu ambao walikuwa wakubwa kidogo walinipenda, shemeji zangu walikuwa wadogo hivyo walikuwa wakiniheshimu na mpaka sasa wananiheshimu.


Lakini hali ya mule ndani haikunifurahisha, kila kitu tulikuwa tukimtegemea mume wangu na kama unavyojua mishahara ya serikali haitoshi.


Yani mimi, Mama mkwe ambaye hakuwa mzee sana, wifi yangu mkubwa ambaye alikuwa ameacha shule kidato cha tatu baada ya kupewa ujauzito na kutelekezwa na mwanae, wifi yangu mwingine ambaye alikuwa kidato cha nne na shemeji zangu wawili ambao mmoja alikuwa kidato cha kwanza na mwingine darasa la sita, tulikuwa ni kula na kulala tu.


Nilimuonea huruma mume wangu ndipo nilipo muomba mtaji wa kufanyia biashara, hapo ndipo mambo yalipoanza kuharibika. Alinipa mtaji wa shilingi laki moja (kipindi hicho laki moja ilikuwa hela nyingi kidogo) na nikaanza kuuza mayai ya kisasa kwa bei ya jumla na rejareja.


Nilitaka kufanya biashara ya mayai nikiwa na lengo la kufuga kuku kwani kabla ya kuolewa nilikuwa nikiishi na shangazi yangu (ndiye aliyenileta Dar)ambaye alikuwa akifuga kuku na niliona kiasi cha fedha alichokuwa akiingiza hivyo kutamani kufanya ile biashara kwani nilishapata kauzoefu kidogo.


Wakati huo huo nilijenga banda dogo la kuku pale nyumbani kwani kulikuwa na uwanja mkubwa na kuanza kufuga kuku wa mayai. Kila kitu nilikuwa nikifanya mwenyewe si Mama mkwe wala wifi zangu walionisaidia ingawa Mama mkwe na wifi mkubwa walikuwa tu pale nyumbani.


Wakati huo nilikuwa na ujauzito wa mtoto wangu wa kwanza. Baada ya kuanza biashara na kuanza kuingiza vipesa kidogo mambo yalibadilika, mwanzoni kazi za nyumbani tulikuwa tukisaidiana ila baada ya kuanza biashara kazi zote walikuwa wakiniachia mimi.


Sikuongea lakini kila siku Mama mkwe alikuwa akiongea kuwa kazi ya mwanamke ni kumuhudumia mume wake, alikuwa akiongea kwa mafumbo na mara kadhaa alimuonya mume wangu kuwa huyu mwanamke atakuja kukutawala akipata pesa.


Mwanzoni mume wangu alikuwa akipuuzia kwani kufanya kwangu kazi kulikuwa kukimpa unafuu wa maisha, angalau sasa aliweza kununua shati lingine kwani kusema kweli faida ilikuwa kubwa na namna nilivyokuwa naweza kuongea na wateja basi ilisaidia.


Pia shangazi yangu ambaye alikuwa mfanyabishara mkubwa aliniunganisha na baadhi ya wateja wake na mara kadhaa alikuwa akinikopesha mzigo mkubwa. Nilipata pesa na kujenga mabanda mawili makubwa na kuanza kufuga na kuku wa nyama.


Kazi zilinizidi ukichanganya na ujauzito ambao nilikuwa nakaribia kujifungua pamoja na ugumu wa kuhudumia kuku nilikuwa nahitaji msaidizi, nilimuomba wifi yangu anisaidie katika kuhudumia lakini alikataa akisema siwezi kumtumikisha kama mfanyakazi. 


Niliongea na mume wangu ambaye alimlazimisha kufanya ile kazi kwani hakuwa akifanya kazi yoyote wakati alikuwa akila bure yeye na mwanae. Hilo lilizua balaa kubwa kwa Mama mkwe akisema nimemtawala mtoto wake namuendesha.


Maneno yalikuwa mengi kwakweli lakini nilivumilia kwani mume wangu alikuwa upande wangu, kila wakati aliniambia kuwapuuza tu. Na mimi nilimsikiliza hivyo niliyasikiliza maneno yao na kuyapuzia.


*****


Maisha yaliendelea na miezi tisa ilifika, sijui niseme kwa bahati mbaya au niseme tu kwa mipango ya Mungu nilijifungua kwa njia ya upasuaji hivyo nilitakiwa kupumzika, lakini nikiwa kitandani nahangaika na mshono kuku walianza kufa mmoja mmoja


Wifi yangu hakuwa akiwahudumia na kama mnavyojua kuku wa kisasa wakikaa na uchafu kidogo tuu basi wanakufa wote. Walianza kufa mmoja mmoja na ndani ya wiki moja kuku zaidi ya hamsini walikufa.


Cha ajabu hakuna aliyekuwa akijali hata mume wangu alikuwa hajali, kitu ambacho kilinishtua zaidi kuliko kile cha kuku kufa. Sikujua nini kilikuwa kimembadilisha mume wangu haraka haraka hivyo hasa baada ya mimi kujifungua, ni kama alikuwa hataki kujihusisha na mimi kabisa wala mtoto. 


Taratibu nilianza kusikia maneno kuwa mume wangu alikasirika kwani mtoto hakufanana na yeye na kulikuwa na maneno kuwa mtoto si wake, mimi na mume wangu ni weusi lakini mtoto alizaliwa mweupe. Sikuwa na cha kusema lakini ukweli nilikuwa nikiujua mimi na Mungu wangu.


Nilivumilia ile hali na pamoja na mshono wangu nililazimika kunyanyuka na kuhudumia kuku wachache wa chotara waliokuwa wamebaki huku nikijipikia na kufua mwenyewe. Nilitamani hata ningekuwa na mdogo wangu wa kike ningemuita anisaidie kwani hawakuwa wakinisaidia chochote.


Nakumbuka mara kadhaa kidonda kilifumuka na kutoa damu lakini nilijikaza hivyo hivyo, ilikuwa ni lazima nifanye zile kazi kwani mbali na kuku lakini hata nguo za mtoto nilifua mwenyewe na nisingefanya hivyo angekosa za kuvaa, hata uji nilikuwa nikijipikia mwenyewe.


Kwa kifupi familia nzima ilinitenga na mume wangu alikuwa ni kama adui tu. Kumbuka huo ndiyo ulikuwa uzazi wangu wa kwanza hivyo nilikuwa sijui chochote. Siku pekee ambazo nilikuwa nikipumzika ni zile ambazo shangazi yangu ambaye naye alikuwa bize sana na kazi zake alikuwa akija kunisalimia.


Hapo hata wao walijifanya kunisaidia kazi na kucheka naye. Yeye ndiyo alikuwa ndugu yangu pekee Dar, wengine walikuwa kijijini, kama ambavyo nilifundishwa uvumilivu katika ndoa sikumuambia chochote na mimi niliigiza furaha.


Maisha yaliendelea lakini hali ilizidi kuwa ngumu, mume alikuwa hatoi pesa ya matumizi na kila nikimuuliza alisema pesa si ninazo na hawezi kutoa wakati hajui hata mtoto ni wanani? Sijui alilipata wapi hilo wazo lakini ndiyo ulikuwa kama wimbo mule ndani, yeye na ndugu zake walikuwa wakiongea kimafumbo kuhusu mwanangu.


Nilivumilia kwani nilijua kuwa ni wake na si wa mwanaume mwingine, ingawa mume wangu alizidi kuwa na hasira hasa mtoto anapolia. Aliongea akisema watoto wa kwao hawalii hivyo huku akiungwa mkono na Mama mkwe, kusema kweli nilichanganyikiwa na nilikuwa sijui cha kufanya.


Siku moja nikiwa katika banda la kuku nasafisha, kuku wote wa kisasa zaidi ya mia mbili wa nyama na wa mayai hamsini walikufa kipindi nimejifungua hivyo nilibaki na mabanda tu na kuku ishirini wa chotara.


Nilisikia kelele za mwanangu akilia kwa nguvu kisha akanyamaza ghafla, sijui kwanini lakini kilio kilikuwa ni tofauti kabisa na siku nyingine na kikubwa ukilinganisha na umri wake. Alilia tu ghafla kwa sauti ya juu na kunyamaza, kusema kweli nilikuwa sijawahi kumsikia akilia hivyo wala kusikia mtoto mdogo akilia hivyo.


Kama chizi nilinza kukimbia kuelekea chumbani nilikokuwa nimemlaza, nilikimbia kwa kasi ya ajabu na nguvu nyingi, mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani, niliugonga sana huku nikiusukuma kwa nguvu, sikujua ni nani ameufunga kwani wakati natoka mume wangu alikuwa bado hajarudi.


Ndugu zake walikuwa hawaingii chumbani kwangu hata kama mtoto akilia namna gani? Kama sipo wanamuacha hivyo hivyo mpaka anyamaze mwenyewe, tofauti na shemeji zangu wifi na Mama mkwe walikuwa hawanisaidii chochote.


Nilipiga mlango kwa nguvu na kama dakika moja hivi ulifunguliwa, alikuwa ni mume wangu akihema kwa nguvu “Nini wewe mbona unataka kunivunjia mlango?” Aliniongelesha huku akinisukuma pembeni.


Alionekana kuwa na wasiwasi sana huku akiangalia angalia pembeni kama mwizi! Sikumjali nilikimbilia kitandani mwanangu alipokuwa amelala, neti ilikuwa imeondolewa, kitanda kimevurugika sana na mtoto amelala chali halii wala hasogei.


“Umemfanya nini mwanangu? Umemfanya nini mwanangu? Umemfanya nini mwanangu? Nilianza kupiga kelele huku nikimuangalia mapigo yake ya moyo kuona kama anapumua nilijikuta napiga ukunga kwa nguvu..!


Mwanangu alikuwa hapumui wala hajitingishi. Nilimuacha pale kitandani na kutaka kutoka nje kumkimbilia mume wangu ili aniambie kamfanya nini, lakini nilipofika mlangoni nilikumbuka namna ambavyo watu hufanya kwenye sinema pale ambapo mtu anakuwa hapumui.


Niliinama na kuanza kumpulizia mwanangu hewa mdomoni kwa kama dakika moja hivi lakini wapi hakupumua. Akili ilisimama kabisa sikujua nifanye nini, nilihisi kama mwanangu alikuwa amefariki, akili yangu ikiwaza kuna kitu ambacho mume wangu alikuwa amemfanyia.


Sikutaka kukata tamaa, nilimnyanyua juujuu na kumning’iniza kichwa chini miguu juu, kusema kweli sikuwa nikijua nafanya nini lakini nilikumbuka namna ambavyo mtoto anayezaliwa anapokuwa halii anavyofanywa, haikusaidia. Nilianza kuwa kama chizi sasa nikifanya kila kitu ambacho niliona kama kingemsaidia kupumua.


Unadhani nini kimetokea? 

Credit; IDD Makengo

ITAENDELEA….

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 

 

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top