(ILIPOISHIA; Mume wangu aliniambia kama naondoka niondoke na kumuachia watoto, alimuambia mwanangu aliyekuwa akilia kuwa simjali hivyo atulie kwani naondoka namuacha…
ENDELEA…..
Kusema kweli sikuwa na cha kufanya, kwa namna yoyote ile nisingeweza kuondoka na kumuacha mwanangu pale, nilijua lazima atateseka sana na nilikuwa tayari kufa kwaajili yake.
Taratibu nilianza kuzirudisha nguo kabatini, ilikuwa asubuhi hivyo nilipaswa kwenda kutayarisha chai, nilijaribu kunyanyuka kutoka pale kitandani lakini nilishindwa, maumivu ya kipigo cha jana yake niliyasikia mpaka mfupa wa mwisho.
Kila sehemu ya mwili wangu ilikuwa inauma hasa tumboni. Ghafla ndipo nilipokumbuka kuwa nilikuwa mjamzito, kusema kweli nilisahau kwa muda nikiwaza mambo mengine. Kwakile kipigo nilihisi kitu kibaya kilikuwa kimetokea, nilikuwa na wasiwasi sana na nilitaka kwenda hospitali ili kuangaliwa.
Nilichukua pochi yangu nikajilazimisha kunyanyuka na kutoka kutaka kwenda hospitalini lakini nilimkuta mume wangu kakaa sebuleni kwenye meza ya chakula.
“Nasubiri chai au unataka niingie jikoni nikajipikie?” Aliuliza kwa dharau, mwanangu alikuwa amekaa pembeni yake analia.
“Huyu naye anatakiwa kwenda shule, unataka nikamuandae mimi?” Nilimuangalia mume wangu na kutamani kufungua mdomo lakini niliogopa kipigo, nilikuwa kwenye maumivu makali na sikutaka kumtukana tena akanipiga.
Nikiwa nawaza nini cha kufanya alitokea Mama mkwe na beseni lenye vitafunwa na chai, kwa mara ya kwanza nilimuona akipika kitu mule ndani.
“Nimekuandalia chai mwanangu, huyu mchawi asije kukuua bure..” Aliongea huku akiniangalia kwa dharau, nilimshukuru Mungu kafanya vile kwani sikuwa na nguvu hata ya kunyanyua kikombe.
“Mjukuu wangu twende nikakuandae” Aliongea akimshika mwanangu mkono. Mwanangu alikataa lakini Baba yake alimuangalia kwa hasira na kwa uoga alienda.
Ingawa sikutaka amguse mwanangu lakini nilishukuru kimoyomoyo kwa kunisaidia.
“Naenda hospitali..” Nilimuaga mume wangu.
“Unaenda kufanya nini? Kuna kliniki leo?” Aliniuliza kwa dharau huku akinywa chai taratibu.
“Hapana naenda kucheki tu afya yangu..” Nilijibu kwa uoga kwani aliacha kunywa chai na kunyanyuka.
“Hakuna cha afya wala nini, najua unachotaka kufanya, unataka ukaongee huko kuwa umepigwa? Sasa hutoki humu ndani wiki nzima!” Aliongea kwa hasira, nilijaribu kujitetea lakini alitishia kunipiga na kuniambia nirejee chumbani.
Inakujia hivi karibuni! |
Kwa uoga nilijikuta naingia chumbani bila kupenda, nilibakia na maumivu nikiwa sijui hatma ya mwanangu tumboni. Mume wangu hakuishia kuniambia tu nikae ndani lakini pia alikuja na kufungia mlango kwa nje, alinifungulia jioni alipotoka kazini na ndiyo wakati nilipopewa chakula mchana wote nilishinda na njaa na maumivu yangu.
*****
Naamini ni miujiza ambayo ilitokea, mimba niliyokuwa nayo haikuharibika na niliendelea na maisha yale mpaka nilipojifungua. Safari hii namshukuru Mungu sikujifungua kwa kisu lakini kama ilivyokuwa mwanzoni baada tu ya kujifungua nililazimika kufanya kila kitu mimi mwenyewe.
Nilifanikiwa kwenda nyumbani na kumueleza Mama matatizo ya ndoa yangu, jibu lake lilikuwa lile lile “Vumilia mwanangu ndiyo maisha ya ndoa yalivyo…” Kusema kweli ilizidi kunikatisha tamaa.
“Hata mimi na Baba yako tumefika hapa kwa kuvumiliana, haikuwa mteremko…” Niliishia tu kumuangalia mama bila kupata kitu cha kumjibu.
Nilijikita tu katika biashara na huko ndipo ilipokuwa faraja yangu, kuongea na wateja kutabasamu ilinisiadia sana. Tulifanikiwa kujenga nyumba nyingine mbili kwa biashara ile, mume wangu alijifanya kuisimamia lakini kila akikaa dukani wiki mbili basi huniita na kunirudisha kwani anaishia tu kupata hasara.
Mwanzoni alipoona biashara inaingiza pesa nyingi aliamua kuacha kazi ili kuisimamia mwenyewe lakini alishindwa hivyo ingawa hakurudi kazini lakini aliniachia nisimamie mimi na yeye ni kuchukua pesa.
*****
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yangu na nilishayazoea. Kupigwa ilikuwa kama sehemu ya maisha yangu. Ingawa tulikuwa na nyumba tatu lakini ndugu zake hawakuondoka, kila tukihama walihama na sisi, kwa kifupi walituganda, shemeji zangu wote walikuwa shule ila wifi zangu wote walishindwa na shule na walishazalishwa wakiwa hawana kazi na watoto wao pale nyumbani.
Nilishaizoea ile hali na nilianza kuona kama kawaida. Siku moja nikiwa dukani mume wangu alikuja kutaka pesa, ilikuwa ni mchana lakini nilikuwa sijauza chochote na pesa zote alizichukua jana yake, nilimuambia hakuna pesa na bila hata kusikiliza maelezo alianza tu kunipiga akisema natumia pesa zake kuhonga wanaume ndiyo maana biashara inafilisika.
Kweli biashara ilishaanza kuyumba lakini sababu kubwa ni kuwa kila mtu alikuwa ni bosi, ndugu zake wakichukua pesa wanavyojisikia, yeye akichukua anavyojisikia na hata Mama yake akichukua anavyojisikia.
Alinipiga sana, majirani hawakuingilia kwani walishazoea ile hali, walikuwa wakiniona napigwa na kunishauri niondoke lakini kila nikifikiria wanangu nilishindwa. Mume wangu alishajua kuwa mimi ndiyo kila kitu katika ile biashara hivyo pamoja na manyanyaso yote lakini alitaka niendelee kuwepo pale.
Alishaacha kazi hivyo kama biashara ingekufa ilimaanisha kuwa wasingeweza hata kupata pesa ya kula. Hivyo kila nilipokuwa nikisema nataka kuondoka alinitishia kuwa atawaua watoto na kweli nilimuamini kwani nilipokuwa nikilalamika angeweza kuwapiga bila sababu ili tu nimuone kuwa ni mkatili anaweza kuwaua kweli hivyo niliamua tu kukaa kimya.
Wakati ananipiga kulikuwa na Mama mmoja mtu mzima anapita zake, aliona namna nilivyokuwa nikipigwa na kuja pale dukani akikimbia.
“Hivi kuna wanaume kweli hapa, mnaona mwanamke anapigwa mpo tu!” Alifoka yule Mama huku akitupa mkoba wake chini na kuja, akaingia ndani kabisa ya duka na kuanza kumsihi mume wangu aniache.
“Wewe Mama haya ni mambo ya familia hayakuhusu!” Mume wangu alimjibu huku akijaribu kumsukuma. Lakini yule Mama hakutingishika, sijui alifanyaje lakini alimkamata mume wangu mkono na baada ya kama sekunde mbili nilisikia mume wangu akipiga kelele za maumivu.
Yule Mama hakumuachia aliendelea kuuminya mkono wake, mume wangu alijaribu kugeuka kumkabili lakini Mama alimkunjakunja, hakumpiga aliendelea kumminya tu mkono, sasa akiwa ameshikilia kiganja tu kama watu wanaosalimiana, aliuminya sana, mume wangu alipiga kelele kwa nguvu kuomba msamaha lakini wapi.
Yule Mama sasa alianza kumvuta mpaka nje, watu walianza kujazana baada ya kuona Mama mtu mzima kama yule miaka kama 65 hivi akimpigisha mume wangu kelele kwa kumshika mkono tu.
Mama wa watu hata hakuongea chochote alimminya tu na mpaka mume wnagu akaanza kujikojolea kama mtoto, kusema kweli pamoja na maumivu niliyokuwa nayo nilijikuta nacheka. Watu walikuwa wakishangilia. Hakuna aliyeingilia na yule Mama hakumuachia, mume wangu alilia kama mtoto nahisi hasa ata alijisaidia ingawa mkojo ndiyo ulionekana ukitiririka huku akilia.
“Sasa piga magoti muombe msamaha mke wako?” Yule mama aliongea huku akimuachia, kiburi chote kilimuishia na mume wangu ambaye ni mrefu na mwenye mwili uliojazia vizuri kimazoezi alipiga magoti mbele yangu na kuomba msamaha. Sikujua hata cha kusema.
“Wanawake hawapigwi pigwi hovyo! Ondoka hapa!” Aliongea yule Mama akimsukuma mume wangu, kwa aibu mume wangu alinyanyuka na kupita katikati ya kundi la watu na kuiingia kwenye gari kisha akatokomea kwa aibu. Nilibaki natetemeka tu kwa furaha, yule Mama hakuongea sana, alinifuata na kuniomba karatasi, kisha akaandika namba ya simu akasema.
“Siku akikugusa tena piga namba hiyo…”
Bila hata kujitambulisha aliondoka zake na kueendelea na safari zake. Kila mtu alikuwa akishangilia wakati Mama yule ambaye hakuonekana kabisa kama mtu wa mazoezi na mwili wake mnene wa kizeezee alifanya kitu ambacho wanaume wengi walishindwa kukifanya.
Sikutaka kusubiri nipigwe ndiyo nipige ile namba, nilijua kabisa siku ile mume wangu angeniua kwa jinsi alivyokuwa amedhalilishwa. Nilijua ile namba ni ya yule Mama kumbe ilikuwa ni ya Mama mwingine (Mungu amrehemu kwani ameshatangulia mbele za haki). Yeye alikuwa ni askari wa jeshi la polisi kitengo cha jinsia.
Nilimpigia na kumuambia mtu aliyenipa ile namba ya simu na mkasa uliotokea. Ilikuwa ni namba yake binafsi na wakati huo hakuwa ofisini lakini aliniomba tuonane, alinielekeza mpaka kwake na nilimuambia mkasa mzima wa maisha yangu.
Aliniuliza ninachotaka nikamuambia kuwa ninataka kuondoka lakini na wanangu, aliniambia ukweli kwakuwa mtoto wangu wa kwanza ana umri zaidi ya miaka saba hivyo anaweza kupewa Baba yake, nilimuambia siwezi kuondoka bila mtoto na yeye akasema kuwa atanisaidia.
Aliniambia kuwa yule Mama aliyenisaidia alikuwa ni dada yake na alikuwa mwanajeshi sasa amestaafu alikuwa na cheo kikubwa tu jeshini. Hapo ndipo nilipoelewa kwanini mume wangu hakufurukuta mbele yake.
Aliniambia niende nyumbani na kama mume wangu akinitishia tu basi vijana wake watakuwa tayari kuja kama nikiwapigia simu. Nilienda kweli na kama nilivyotarajia mume wangu alikuwa akinisubiri kwa hamu, nilipofika alianza kunipiga, nilipambana nikajitoa mikononi mwake kisha nikakimbilia chumbani na kujifungia kwa ndani kisha nikapiga ile namba niliyopewa na dakika kadhaa askari walikuja.
Sikujua lakini kumbe waliambiwa wanifuate, walimkamata mume wangu wakati ananipiga na kumuweka ndani. Alifunguliwa shitaka la kupiga na kujeruhi. Wakati kesi ikiendelea kukiwa na uwezekano mkubwa wa yeye kufungwa aliniomba msamaha, sikuwa tayari kumsamehe lakini sikuwa na namna.
Alikubali kuwaacha watoto chini yangu (kwa kuandikishana kabisa) kitu ambacho nilikuwa nikikitaka na sisi kugawana mali zote tulizochuma pamoja nusu kwa nusu. Nilitaka kukataa lakini wakili wangu alinishauri nikubali kwani hata kama angefungwa lakini akitoka ningeweza kukosa kila kitu.
Mali zote ambazo tulichuma na mume wangu alikuwa ameandika majina ya Mama yake hivyo hazikuwa zetu, kwa maana hiyo kama nigemuacha afungwe basi nisingeondoka na kitu kwani nyumba kisheria hazikuwa zetu bali za Mama yake.
Kwakuwa pia sikutaka kuendelea kumuona nilikubali, tukagawana kila kitu sawa na tukafanya mpango kesi ikafutwa huku nikifungua kesi nyingine ya kudai talaka nikapata talaka mahakamani.
Huu ni mwaka wa tatu sasa ninaishi peke yangu na wanangu, duka ambalo mume wangu alilichukua lilishafungwa kwani hakuna kitu, mimi nilifungua duka jingine na kuhama na wateja wote. Sasa nimejenga nyumba nyingine ambayo naitumia kufuga kuku ambapo nina kuku zaidi ya elfu kumi.
Sina mawasiliano kabisa na mume wangu kwani hata kupiga simu kuwajulia hali watoto hataki, nasikia tu sasa hivi wameshauza nyumba moja ambayo tuligawana ile ambayo tulijenga pamoja na ile ambayo ilikuwa ya familia tuliyoikarabati wamepangisha na wamebaki na vyumba viwili tu yeye na dada zake kwani hana kazi na wote hawana kazi.
Nashukuru Mungu nilitoka lakini nawaelewa kuna wanawake wengi ambao bado wako kwenye ndoa za mateso. Kuna uoga mkubwa wa kutoka, kuna ile kuwaza maisha yatakuwaje na vipi kuhusu watoto na upuuzi mwingine wa kuwaza labda atabadilika labda kesho itakuwa tofauti.
Niwashauri kitu kimoja, akikupiga nenda kamshitaki, kuna dawati la jinsia karibu katika kila kituo cha polisi, anzia hapo, katoe taarifa na anawatishia mpaka watoto akiwatumia kukunyanyasa. Ukikosa msaada nenda kituo kikubwa na ukikosa nenda maendeleo ya jamii na hata kwa mkuu wa wilaya fika.
Itakusaidia sana kama huko mbeleni akitaka kuwang’ang’ania, hata mkifika mahakamani wataamua watoto kukaa sehemu ambayo watakuwa salama zaidi. Usikae tu ndani na kuishia kulalamika kwa ndugu, wataishia kukuambia tu uvumilie mpaka pale atakapokuua. Kuna wanawake wengi huvumilia makubwa zaidi ya haya na huogopa kutoka.
Usivumilie na acha kuwasikiliza ndugu ambao kazi ni kukuambia vumilia na kukuogopesha kuwa maisha hayaendi bila mwanaume. Vumilia kila kitu lakini si kipigo na manyanyaso. Nimevumilia mengi na natamani ningekutana na yule Mama mwanzo kabisa wa ndoa yangu ningeweza kutoka mapema. Ahsanteni kwa kusoma kisa changu na Mungu awabariki natumaini mmejifunza.
***TIPS***
Wanawake wengi wanalazimika kuvumilia ndoa za mateso kwaajili ya watoto, wanaona kama wakiondoka basi watoto wao watateseka kwa mwanaume ambaye alikuwa mnyama kwao au kupata Mama wa kambo na kuwatesa.
Kitu ambacho hawajui ni kuwa wanaweza kuwatumia watoto haohao kuleta upendo ndani ya nyumba zao na kuwabadilisha hao wanaume. Kujua namna ya kuwatumia watoto kumbadilisha mume wako soma kitabu cha “ndoa Yangu Furaha Yangu” Ni shilingi elfu 9,999/- tu na kinapatikana kupitia simu yako. Kukipata tuwasiliane 0742-381-155 au 0657-552-222.
*MWISHO*