Mshukiwa aliyeshtakiwa kwa wizi katika Kituo cha Polisi cha Kathiani, Kaunti ya Machakos nchini Kenya amewabwagia nyuki maafisa wa polisi katika jaribio la kutoroka kizuizini.
Katika ripoti ya polisi, iliripotiwa kuwa nyuki hao mara ya kwanza walimvamia afisa mmoja aliyekuwa akifungua selo ya mshukiwa mnamo Jumatano, Mei 4,2022.
Kabla ya tukio hilo mshukiwa alimtupia uchafu afisa mmoja aliyefahamika kwa jina la David Mambo aliyekuwa akimfunga pingu.
“Mshukiwa alimtupia uchafu na mara nyuki hao walianza kuwavamia askari huku mshukiwa akijaribu kutoka nje lakini askari waliwavumilia nyuki hao na kufanikiwa kumfunga pingu mshukiwa,” ripoti ya polisi ilieleza.
Polisi hao waliongeza kuwa maafisa wengine wanne waliokuwa wamefika katika eneo la tukio ili kumuokoa mwenzao walipelekwa katika hospitali ya Kathiani Level 4 na wanauguza majeraha ya kuumwa na nyuki.
Maafisa hao wa polisi wa Machakos walidokeza kuwa wanachunguza kisa hicho ili kubaini jinsi nyuki waliingia selo zao bila wao kujua.