Wajawazito katika Zahanati ya Chibe Manispaa ya Shinyanga, wamedaiwa kujifungua katika jengo moja na wagonjwa wa kawaida.
Imedaiwa kuwa wajawazito hao wanapokuwa wanajifungua na kupiga kelele, husikiwa na wagonjwa na maneno ambayo huyatoa wanapokuwa wakisukuma watoto sababu ya uchungu, wagonjwa huanza kuwajibu.
Diwani wa Chibe, John Kisandu, amebainisha hayo leo kwenye kikao cha Baraza la Madiwani Manispaa ya Shinyanga, wakati akiwasilisha taarifa ya kata hiyo.
Amesema wajawazito katika Zahanati ya Chibe wamekuwa wakipata shida wakati wa kujifungua, sababu ya kutumia jengo moja na wagonjwa, ambao huwasikia wakati wa kujifungua na kuanza kujibizana maneno ambayo huyatoa jambo ambalo si zuri.

“Zahanati ya Chibe ina jengo moja tu hilohilo lihahudumia wagonjwa na kujifungua wajawazito. Naomba sana hili liangaliwe na kujengwa jengo lingine kwa ajili ya kujifungua kinamama tu,” amesema Kisandu.
“Siku moja nilikuwa nikipata matibabu katika zahanati hiyo, nikasikia mwanamke akilia kwa uchungu wakati akijifungua huku akitamka maneno kuwa wanaume wote wauawe, lakini wanawake wenzake walianza kumjibu kuwa auawe wa kwako tu,” ameongeza Kisandu.

Nao madiwani walipokuwa wakiwasilisha taarifa zao za kila kata, wamelalamikia kukabiliwa na tatizo la ukamilishaji wa maboma ya afya, uchakavu miundombinu ya shule, barabara, matundu ya vyoo pamoja na uhaba wa watumishi.
Naye Meya wa Manispaa wa Manispaa ya Shinyanga, Elias Masumbuko, amesema kero zote ambazo zimewasilishwa na madiwani kupitia taarifa zao za kwenye kata zifanyiwe kazi.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Jomaary Satura, amesema tatizo ambalo linakwamisha utatuzi wa kero hizo ni upungufu wa rasilimali fedha na kubainisha kuwa watakuwa wakizitatua moja baada ya nyingine, na hadi kufikia mwaka 2025 nyingi zitakuwa zimeshatatuliwa.
Credit;Nipashe