Wananchi hao wamebandika mabango katika ofisi hiyo ya kijiji, yenye jumbe mbalimbali ikiwamo ya kutaka mtendaji na mwenyekiti wa kijiji waondolewe.
Wamedai kuwa wanashinikiza viongozi hao kuondolewa kutokana na ubadhilifu wa Sh19 milioni ambazo matumizi yake hayajulikani.
Wakizungumza leo Jumatatu Mei 9, 2022 wananchi hao wamedai kuwa mkutano wa mwisho kuitishwa kijijini hapo ni mwaka 2015 ambao ulivurugika baada ya wananchi kuhoji fedha zitokanazo na mashamba ya kijiji ya mpunga.
Kwa upande wake mwenyekiti Kijiji hicho, Elibariki Molla amekiri kufungwa kwa ofisi hiyo na kwamba akisema kuwa imefungwa na baadhi wananchi ambao hawataki maendeleo ya kijiji.
"Mgogoro huu upo kwa mkuu wa wilaya na unashughulikiwa huko hivyo wanatakiwa kuwa na subira na uamuzi mzuri utatoka kwa Mkuu wa Wilaya ambako ndiko walipeleka barua za malalamiko" amesema
Mtendaji wa kijiji cha Rau River, Mary Kundya amesema hana taarifa za kufungwa kwa ofisi na yuko nyumbani kwa matatizo ya kiafya.
Diwani wa Kata ya Kahe Magharibi, Aloyce Mumburi amesema malalamkiko ya wananchi ni ya kweli na kwamba kijiji hicho hakijawahi kufanya mikutano ya kijiji kwa muda mrefu na kuwataka wenyeviti wa vijiji kufutata taratibu na sheria za kuongoza wananchi.
"Kimsingi watendaji washauri vyema wenyeviti wa vijiji kuhusu swala la kiserikali la uitishwaji wa mikutano ya kijiji pia Mkurugenzi mtendaji kuandaa semina elekezi kwa wenyeviti wa vijiji ili waweze kutimiza majukumu yao na kuondokana na migogoro ya wananchi" amesema
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Moshi, Kastory Msigala amesema wananchi kufunga ofisi ni kosa kisheria kwa kuwa wapo baadhi ya wananchi wanahitaji huduma na kwamba anafuatilia kujua sababu iliyopelekea hadi wafikie uamuzi huo.