Wanafunzi kutoka Skuli sita Kisiwani Pemba walioshiriki katika mashindano ya kipima uelewa juu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi, afya ya Uzazi pamoja na Stadi za maisha wameombwa kuwa mabalozi wazuri kwa jamii kutokana na elimu walioipata kupitia mashindano hayo ili waweze kuepukana na madhara mbali mbali yanaweza kujitokeza.Picha zaidi tazama chini hapo.
Mapema akikabidhi zawadi kwa Skuli tatu zilizofanya vizuri kwenye mashindano hayo, Afisa mdhamin kutoka ofisi ya makamo wa kwanza wa Rais Ahmed Abuubakar Mohammed, amesema lengo la mashindano hayo ni kujenga uelewa juu ya masuala mazima ya kujikinga na virusi vya Ukimwi, elimu ya afya ya uzazi pamoja na Stadi za Maisha.
Aidha, amewaomba waalimu wa Skuli hizo zilizoshiriki mashindo hayo kuanzisha Klabu zinazotoa elimu juu ya kujikinga na Virusi vya Ukimwi ili kuhakikisha wanafunzi wanapata fursa ya kuongeza uelewa wa namna ya kujinga na janga hilo.
‘’
Kwahivyo niwaombe mukawe mabalozi wazuri kwa wanafunzi wenzenu na jamii kwa ujumla napia niwaombe waalimu muziimarishe zile klabu za HIV na VVU katika shule zenu ili kuengeza uelewa kwa vijana na jamii zilizotuzunguka’’ alieleza
Kwa upande wake, Kaimu mratibu wa tume ya Ukimwi Pemba Ali Mbarouk, amesema wameamua kutoa mafunzo hayo kwa wanafunzi hao kwasababu rika la vijana ndio rika pekee ambalo kwa kiasi kikubwa ndilo ambalo ambalo huathiriwa na mabadiliko mbali mbali ya kitabia.
‘’Kama tunavyojua kuwa rika la ujana ndio rika ambalo linashawishi kufanya kila kitu na mara nyingi ni rika ambalo halishawishi mambo mazuri most time linashawishi mambo maovu kama vile kujiingiza katika vitendo vya uhasharati, kutumia vilevi, kubaka nakadhalika, hivyo basi tume ya ukimwi zanzibar ikaona kuna haja ya kuandaa program ya kukutana na rika hili ili kulipa taaluma juu ya maambukizi ya virusi vya HIV, Afya ya Uzazi na Stadi za Maisha ili waweze kujitambua’’ alifafanua
Nae, Mkuu wa Idara ya Uratibu Kinga kutoka Tume ya Ukimwi Zanzibar Sihaba Saadati Iddi, amesema utafiti uliofanywa na Wizara ya Afya Zanzibar kwa kushirikiana na tume ya Ukimwi inaonesha takriban Wazanzibar (7647) wameambukiwa Virusi vya Ukimwi sawa na asilimia 0.4 kwa kujibu wa Sensa ya idadi ya watu wa Zanzibar ya mwaka 2012 ambapo kati yao wanaume ni 3010 na wanawake ni 4636.
‘’Hatua ambazo tumezichukua wadau mbali mbali, tume ya Ukimwi NA Wizara ya Afya zinaonesha kiwango chetu cha maambukizi ni sio kikubwa cha kutisha kulinganisha na nchi nyengine’’ alisema
Abdalla Omar Hassan ni muezeshaji kutoka Wizara ya Afya kitengo shirikishi cha Ukimwi Pemba, amesema miongoni mwa sababu zinazopelekea vijana wengi kujiingiza kwenye vitendo viovu ni pamoja na mabadiliko ya mwili, malezi mabaya pamoja makundi rika,hivyo basi amewaomba wazazi kuwa karibu na watoto wao ili kufahamu nyendo zao.
Nao, baadhi ya wanafunzi walioshiriki mashindano hayo pamoja na mafunzo yaliyotolewa wameahidi kuyafanyia kazi mafunzo pamoja na kuyasambaza kwa wengine ili yaweze kuleta tija kwao na jamii kwa ujumla.
‘’Mashindano yalikuwa mazuri sana pamoja na mafunzo pia nimejifunza mambo mengi sana kuhusu virusi vya ukimwi, afya ya uzazi pomoja na stadi za maisha lengo ni kuhakikisha naisambaza elimu kwa wanafunzi wenzangu ili nao waweze kuipata na kutusaidia sote kwa ujuma’’ alisema mmoja wa wanafunzi hao Takwimu ya kitaifa ya mwaka 2016\2017 inaonesha watu wenye umri kati ya miaka 15 hadi 49 ambao wameambukizwa Virusi vya Ukimwi kwa upande wa Tanzania Bara ni 4.7 na kwa upande wa Zanzibar ni 0.4 sawa na Wazanzibari 7647.
Mashindano hayo ya kupima uelewa juu ya Ukimwi, Afya ya uzazi pamoja na Stadi za maisha ni muendelezo wa kampeni ya ‘’KIJANA KATAA UKIMWI’’ ambapo yamejumuisha Skuli sita za Pemba ikiwemo Skuli ya Sekondari Kiwani, Skuli ya Sekondari Uwandani, Skuli ya Sekondari Chwale, Skuli ya Sekondari, Shumba, Skuli ya Sekondari Amini Islamic ya Wesha na Skuli ya Sekondari na Skuli ya Sekondari Mwitani ya Wete, ambapo Skuli ambazo zimeibuka kidedea kwenye mashindano hayo ni pamoja na Skuli ya Sekondari Kiwani ambayo imeshika nafasi ya kwanza, Skuli ya Sekondari Chwale ambayo imeshika nafasi ya pili na Skuli ya Sekondari Amin Islamic ya Wesha ambayo imeshika nafasi ya tatu.