Wananchi wa Mahenge wilayani Ulanga mkoani Morogoro wamelalamikia kitendo cha ngedele/nyani kuvamia hospitali ya wilaya hiyo na kuingia kwenye wodi za wagonjwa kuchukua nguo na vyakula kisha kukimbia navyo msituni.
Wakieleza changamoto hiyo wakati Mbunge wa jimbo la Ulanga Salim Alaudin Hasham alipotembelea katika hospitali hiyo wananchi hao wamemuomba mbunge huyo kuwasaidia kutatua kero hiyo ikiwa ni pamoja na kutengeneza fensi kwa kwa ajili ya usalama.
Kaimu mganga mkuu wa hospitali hiyo Stephan Liwemba amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema ngedele hao wanatoka katika msitu wa Kasita ulipo kilometa chache kutoka katika hospitali hiyo.
Aidha Liwemba amesema tatizo hilo ni la msimu na hutokea mara nyingi kipindi ambacho miti iliyopo hospitalini hapo ikianza kutoa matunda.
Akizungumza na wanachi hao Mbunge wa jimbo la Ulanga Salim Alaudin Hasham licha ya kushangazwa na tukio hilo ameahidi kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo.