Wananchi wa Kijiji cha Mtulingala Kilichopo katika kata ya Kitandililo Halmashauri ya Mji wa Makambako Mkoani Njombe Wamemuomba kibali Mkuu wa Wilaya Ya Njombe Kissa Gwakisa Kasongwa cha Kumfukuza Mwananchi Mwenzao kijijini hapo anayefahamika kwa jina la Abbas Mhelela kwa kile kinachodaiwa kuwa ana vitendo vya kishirikina.
Wakizungumza katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na mkuu huyo wa wilaya kwa lengo la kusikiliza kero mbalimbali wananchi hao wamesema kuwa Abbas amekuwa akiwasumbua kwa muda mrefu kwa kuwapa vitisho vya kuwaroga huku akimzuia mwanae kuendelea na masomo kwa kusema kuwa endapo atakaidi na kuendelea atakapofika kidato cha nne atafariki ama atakuwa kichaa.
Imani Fute ni diwani wa kata hiyo amesema kuwa wananchi wake wamekuwa wakishindwa Kufanya maendeleo kwa Kuhofia mambo ya ushirikina na hata katika sekta ya elimu wanashindwa kufanya vizuri kutokana na imani hizo za kishirikina.
Aidha baada ya kusikiliza kero hiyo ya wananchi mkuu wa wilaya Kissa Gwakisa Kasongwa anatoa agizo kwa wananchi pamoja na wazee wa kijiji hicho huku akilitaka jeshi la polisi kufanya mahojiano na Abbas akiwa chini ya uangalizi.
TAZAMA VIDEO HII WANANCHI WAKIOMBA KIBALI CHA KUMFUKUZA MCHAWI!.