‘ZLSC’ NA ‘FCS’ KUWAPA ELIMU WANANCHI JUU YA UTATUZI WA MIGOGORO KWA NJIA MBADALA YA AMANI NA HAKI.

Hassan Msellem
0

Wananchi Kisiwani Pemba wametakiwa kutumia njia mbadala ya amani na haki katika utatuzi wa migogoro wa kesi za madai ili kuendelea kudumisha amani na haki nchini.



Mapema akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kibubunza Shehia ya Shumba Muhogoni Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba, Afisa programu kutoka taasisi ya Foundation For Civil Society “FCS” Evelyn Mchau, alisema taasisi ya Foundation    For Civil Society kwa kushirikiana na kituo cha huduma za sheria Zanzibar “ZLSC” zimedhamiria kuwajengea uwezo wananchi juu ya namna bora ya utatuzi wa migogoro kwa njia shirikishi na majadiliano ili kuendelea kudumisha amani na haki nchini.

 

Aidha alisema suala la migogoro ni suala linalomgusa kila mmoja katika jamii, hivyo basi amewaomba wananchi hao kuwa na utaratibu nzuri wa usuluhishi katika utatuzi wa migogoro inayowakabili.

 

“Ukichunguza vyanzo vingi vya migogoro mingi katika jamii zetu inatokana wanajamii kutofautiana kisha kushindwa kukaa pamoja wakasuluhisha na badala yake kukimbilia kwenye vyombo vya sheria, niwaombe sana musifanye hivyo pindi munapotofautiana na badala yake kutaneni na musuluhishane wenyewe” Evelyn Mchau



Afisa programu kutoka taasisi ya Foundation For Civil Society 'FCS' Tanzania Evelyn Mchau.

Kwa upande wake, Mratibu wa Kituo cha huduma za sheria Zanzibar upande wa Pemba Safia Saleh Sultan, alisema njia nzuri ya wananchi kuepukana na migogoro na na uvunjifu wa amani ni kukaa pamoja na kusuluhishana wenyewe ili kuepukana na chuki pamoja na visasi.


Ameongeza kuwa, miongoni mwa sababu zinazopelekea kutoweka kwa amani nchini ni uwepo wa migogoro mbali mbali katika jamii ikiwemo migogoro ya ardhi, mashamba pamoja na familia.

 

Alisema “Naomba niwasihi sana ndugu wananchi munapokuwa na migogoro mbali mbali kama vile migogoro ya ardhi, mashamba pamoja na familia kaeni pamoja musuluhishane badala ya kuanza kuchukiana na kuchukuliana sheria mikononi hiyo ni mbaya sana”

 

Mratibu kutoka Kituo Cha huduma za Sheria Zanzibar 'ZLSC' Safia Saleh Sultan.


Nae, wakili kutoka kituo cha huduma za sheria Zanzibar tawi la Pemba Siti Habib Mohammed, aliwasihi wananchi hao kuzifanyia suluhu wenyewe kesi za madai kwani kuzipeleka katika vyombo vya sheria husababisha ugomvi na uhasama.

 

Aidha wakili huyo, alisema amewaasa wana kijiji hao kutokuzifanyia suluhu kesi za jinai ikiwemo kesi za udhalilishaji.

 

“Kwahivyo niwaombe pindi munapokuwa na kesi za madai ni vyema mukasuhisha wenyewe badala ya kupelekana kwenye vyombo sheria ispokuwa kwa kesi za jinai hususan kesi za udhalilishaji” alishauri



Wakili kutoka 'ZLSC' Siti Habib Mohammed.

Ali Abdalla Ameir ni mwananchi wa kijiji hicho, ameomba elimu ya usuluhishi wa migogoro kwa njia ya amani kutolewa mara kwa mara ili wananchi wawe na uwezo nzuri wa kutatua migogoro inayojitokeza kwa njia ya haki na utulivu

 

“Ni washukuru sana kwa ujio wenu kwetu kwakweli tumejifunza mambo mengi sana kuhusiana na sheria na njia bora ya utatuzi wa migogoro kwa njia amani, niwaombe leo isiwe mwisho muwe munakuja mara kwa mara ili wananchi wazidi kupata elimu hii na waweze kuitumia” alishauri


Mwanakijiji Ali Abdalla Ameir akiulizwa maswali Kwa Maafisa wa ZLSC na FCS.


Afisa ufuatiliaji na tathmini kutoka “ZLSC” Zanzibar Khamis Haroun Hamad, amewataka wananchi kushirikiana katika utatuzi wa kesi za madai zinazotokezea katika maeneo yao.

 

Nao baadhi ya wananchi walisema wanakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo changamoto mipaka ya mashamba pamoja na rushwa kwa upande wa kesi za madai.



Khalfan Hamad Juma mwanakijiji.

Akifunga mkutano huo, sheha wa shehia hiyo Salim Said Salim, amawashukuru maafisa kutoka ‘ZLSC’ na ‘FCS’ kwa kuwafikia wananchi hao katika kuwapatia elimu hiyo adhimu ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi.

 

“Kwa niaba ya wananchi wa kijiji cha Kibubunza, niwapongeze watendaji wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’ kwa kuja kwenu kutoa elimu hii kwa wananchi” alieleza



Wa mwanzo kulia aliyesimama Sheha wa Shehia ya Shumba Muhogoni Salim Said Salim.

Akieleza namna ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, mratibu wa ‘ZLSC’ Pemba Safia Saleh Sultan, alisema miongoni mwa njia bora za wananchi kutatua migogoro inayowakabili ni pamoja na kuwatumia wazee, viongozi wa dini, vikao vya familia, watu maarufu pamoja wasaidizi wa huduma za sheria.



Baadhi ya wananchi wakifuatilia Kwa umakini mkutano huo.

Kituo cha huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’ kwa kushirikiana shirika la Search For Common Ground ‘FSC’ wanaendesha mradi wa mwezi mmoja wa utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala za amani na haki,, unaofadhiliwa na na taasisi ya Foundation For Civil Society ‘FSC’.





Wasanii wa kikundi Cha uigizaji wakiigiza igizo juu njia mbadala ya utatuzi wa Migogoro ya familia na Ardhi  Kwa njia ya Amani na Haki.


Mwisho.

 

 

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 


 

 




#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top