JUMWAMPE- YAWAOMBA WALIMU WA MADRASA KUFUNDISHA SOMO LA MAADILI ILI KUPUNGUZA VITENDO VYA UDHALILISHAJI.

Hassan Msellem
0

Walimu wa madrasa wameombwa kufundisha somo la maadili katika madrasa zao na katika jamii ili kupunguza idadi ya matukio ya vitendo vya udhalilishaji nchini.



Mapeama akifungua mafunzo ya siku moja kwa walimu wa madrasa huko katika Skuli ya Sekondari ya Idriss Abdul Wakil Kizimbani Wete Pemba yaliyoandaliwa na jumuiya ya maendeleo ya walimu wa madrasa Pemba 'JUMWAMPE', Mkuu wa Wilaya ya Wete Mhe. Hamad Omar Bakar, amesema kukithiri kwa vitendo vya udhalilishaji kunachangia kwa kiasi kikubwa kuporomoka kwa maadili sambamba na upotevu wa nguvu kazi kwa taifa.

 

Ameongeza kuwa Wilaya ya Wete ni miongoni mwa Wilaya inayoongoza kwa idadi ya matukio ya vitendo vya udhalilishaji kisiwani Pemba huku ikiwa inashika nafasi ya pili visiwani Zanzibar.

 

“Kwahivyo ndugu waalimu nahisi sasa kuna ulazima wa kuanzisha utoaji wa elimu ya maadili ili wanafunzi pamoja na jamii iweze kuifahamu elimu pamoja na kuwa na khofu ya Mungu ili tuweze kupunguza matukio ya udhalilishaji” alishauri


Mkuu wa Wilaya ya Wete Hamad Omar Bakari akizungumza na waalimu wa madrasa walioshiriki katika Mafunzo hayo.


Kwa upande wake, Mkuu wa divisheni ya utawala, mipango na rasilimali watu Said Khalfani Issa, alisema walimu wa madrasa ni watu mihimu katika malezi ya jamii, hivyo basi wanapaswa kujitambua ili waweze kuepukana na vitendo viovu ikiwemo vitendo vya udhalilishaji.

 

“Nyinyi ndio muhimili wa jamii katika mambo mbali mbali ikiwemo kusimamia na tabia za watu katika jamii zetu kwahivyo muna umuhimu mkubwa mno, lakini ili umuhimu huo uonekane munapaswa kujitambua nyinyi ni nani na muna nafasi gani katika jamii” Said Khalfan Issa

 

Akiwasilisha mada juu ya umuhimu wa kuweka kumbukumbu za fedha katika madrasa Khator Ali Abdalla, amewasisitiza waalimu hao kuwa na uwezo mzuri wa kujua hesabati pamoja kuweka kumbukumbu katika uwekaji na matumizi ya fedha ili kuepukana na migogoro inayojitokeza mara kwa mara.

 

Alisema “Tumekuwa tukisikia kesi nyingi sana kuhusu matumizi mabaya ya utumiaji wa fedha katika madrasa, hivyo basi kupitia wasilisho hili nadhani mumejifunza umuhimu na namna bora uwekakaji wa kumbukumbu za fedha ili kuondoka na kesi zinazojitokeza mara kwa mara”

 

Nae, Mkurugenzi wa jumuiya ya Mazingira na Utetezi wa Kijinsia Pemba ‘PEGAO’ Hafidh Abdi Said wakati akiwasilisha mada juu ya Uongozi, alisema ili kiongozi aweze kuwa kiongozi bora anapaswa kuwa na sifa ya kuona mbali, kushirikiana na anaowaongoza, kuwa na moyo wa kujitolea pamoja na kukubali kukosolewa.

 

“Kiujumla kuna sifa nyingi sana zinazomfanya kiongozi kuwa bora kama mulivyozitaja lakini, hizo sifa nne ambazo nimezitaja hapo juu ndio sifa kuu ambazo kiongozi anapaswa kuwa nazo ili nafasi yake ya uongozi aweze kuitumikia iapaswavyowa, kwahivyo nawaomba sana waalimu muzizingatie sifa hizo” Hafidh Abdi Said

 

Aidha aliwasihi waalimu hao kuachana na tabia ya kujibagua na kujiona bora kutokana na kutofautiana na misingi ya kimadhehebu ili kuepukana na migogoro pamoja na mipasuko inayojitokeza mara kwa mara.

 

Hafidh Abdi Said Mkurugenzi wa Jumuiya ya Mazingira na utetezi wa kijinsia Pemba.


Akiwasilisha mada juu ya njia bora za utatuzi wa migogoro Salum Hamad Shaib, aliwaomba waalimu hao kukaa meza moja pindi wanapotofautiana na wazazi na walezi ili kuweza kuitatua migogoro inayojitokeza kwa njia ya amani na haki.

 

Alishauri “Kama tunavyojua kuwa suala la migogoro ni suala ambalo haliwezi kuepukika katika maisha ya mwanadamu, lakini inapotokezea tofauti niwaombe mukae meza moja ili muweze kumaliza tofauti zenu kwa njia ya amani na haki”

 

Salum Hamad Shaib, akiwasilisha Mada juu ya njia bora ya utatuzi wa migogoro kwa njia Amani na Haki.

Akitoa nasaha kwa waalimu hao mwenyekiti wa jumuiya ya maendeleo ya waalimu wa madrasa Pemba Hamad Ali Hamad, amewasihi waalimu hao kuachana na tabia ya kulumbana, kuchukiana sambamba na kuwafanyia husda wanafunzi wao wenye ufahamu nzuri wa masomo ili waweze kupata wasaidizi wazuri katika majukumu yao.

 

Nao, waalimu hao wameahidi kuyafanyia kazi ipaswavyo mafunzo ili yaweze kuwanufaisha wao na jamii kwa ujumla.


Waalimu wa madrasa kutoka Wilaya ya Wete walioshiriki katika Mafunzo hayo ya siku Moja.

Mafunzo hayo ya siku moja yameadaliwa na jumuiya ya maendeleo ya waalimu wa madrasa Pemba ‘JUMAMPWE’ yameshirikisha waalimu wa madrasa 87 kutoka shehia 32 za Wilaya ya Wete Pemba.


Baadhi ya walimu wanawake walioshiriki katika Mafunzo hayo.


Mwisho.

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 


 

 




#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top