Mtu mmoja amefariki na wengine wawili kujeruhiwa katika ajali iliyohusisha Basi la Kampuni ya Sky Line lenye namba T334 DGB lililokuwa linatokea Manyara kuelekea Dar esalam ambalo limegongana uso kwa uso na Toyota Coaster (IT) lenye namba IT 4849 lililokuwa inatokea Dar es salaam kwenda Rwanda .
Ajali hiyo imetokea katika Kijiji cha Mahembu Kata ya Mtumbatu Wilayani Kilosa Mkoani Morogoro, Barabara Kuu ya Morogoro - Dodoma.
Dereva wa Basi la Sky Line, Chesto Lubimbo amesema Basi hilo lilikuwa na abiria 55 na chanzo cha ajali hiyo ni Dereva wa gari la Coaster (IT) kujaribu kuyapita magari yaliyopo mbele yake bila kuchukua tahadhari.
Kamamda wa Polisi Mkoa Morogoro, Fortunatus Musilimu amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo ambapo amemtaja aliyefariki kuwa ni Isack Segiyuva, Raia wa Rwanda ambaye alikuwa Dereva wa Coaster (IT) na majeruhi ni Fundi wa Basi la Sky Line, Daudi Kimaro ambaye amevunjika miguu na Rajabu Lungi ambaye ni abiria.