KUWANYANYAPAA WAHISIWA WA MARADHI YA KUAMBUKIZA KUNASABABISHA KISASI CHA KUSAMBAZA KWA WENGINE- KAIMU MRATIBU TB,HIV ZANZIBAR.

Hassan Msellem
0

Waandishi wa habari Kisiwani Pemba wameombwa kuelimisha jamii juu ya athari zinazotokana na kuwanyanyapaa wahisiwa wa maradhi ya kuambukiza ya Kifua Kikuu, Uviko19 na wanaoishi na Virusa vya Ukimwi ili kuepukana na madhara yatokanayo na kuwanyanyapaa wahisiwa wa maradhi hayo.

 


Mapema Akizungumza na Waandishi wa Habari huko katika Ukumbi wa Maabara ya Afya ya Jamii Wawi, Kaimu Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukimwi Zanzibar, Valeria Rashid Haroub, amesema miongoni mwa sababu zinazosababisha kuongezeka kwa maradhi ya kuambukiza ni tabia ya kuwanyanyapaa wahisiwa wa maradhi hayo hali inayopelekea kuwa na visasi vya kuyaambukiza maradhi hayo kwa wengine.

 

“Takwimu zinaonesha kuwa waathirika wengi wa maradhi ya kuambukiza ikiwemo HIV inatokana na tabia ya kuwanyanyapaa watu walioambukizwa maradhi hayo, jambo ambalo linamfanya aliyeambukizwa wa maradhi hayo kuwaambukiza watu wengine ikiwa ni sehemu ya kulipiza kisasi” Alisema

 

Aidha Bi. Valeria amewaomba wanajamii kuwajali na kuwatunza watu wanaoishi na maradhi ya kuambukiza ili kuwaondoshea hali simanzi, hasira, visasi na upweke.

 

“Niwaombe sana mukawaelimishe wananchi juu ya umuhimu wa kuwajali na kuwatunza watu wanaoishi na maradhi ya kuambukiza kwasababu kitendo cha kumnyanyapaa mtu kinaongoza ugonjwa, simanzi, hasira, kisasi na upweke na ndio maana baadhi ya wahisiwa wa maradhi hayo hufikia pahala wakachukuwa hatua mbaya ikiwemo kulipiza kisasi kwa kuwaambukiza wengine au kujinyonga” Bi. Valeria

 

Akiwasilisha mada juu ya maradhi ya Kfua Kikuu, mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Said Khamis Ahmada, amesema inakisiwa kuwa takribani Wazanzibari 124 kati ya Wazanzibari laki moja wanahisiwa kuugua kifua kikuu sawa na wahisiwa 1,612 kila mwaka.

 

“Kifua kikuu ni ugonjwa magonjwa kumi yanayosababisha vifo vingi duniani, inakisiwa kuwa watu milioni 10 wameugua TB na milioni 1.5 wamefariki kwa ugonjwa kifua kikuu katika mwaka 2020 duniani kote” Said Khamis Ahmada

 

“Takwimu za maradhi ya Kifua Kikuu kwa 2020-2021 za Wilaya zinaonesha Wilaya ya Mjini Magharibi B ndio Mkoa unaongoza kwa wahisiwa wa kifua kikuu kwa kuwa na wahisiwa 163 mwaka 2021 kutoka wahisiwa 124 mwaka 2021 ukifuatiwa na Wilaya ya Wete Pemba kwa kuwa na wahisiwa 140 mwaka 2020 kutoka wahisiwa 105 mwaka 2021” Said Khamis Ahmada

 

“Kwa upande wa takwimu za ugonjwa wa Kifua Kikuu Zanzibar kutoka mwaka 2017 hadi 2021 zinaonesha takriban watu 1090 wamehisiwa kuwa na maradhi ya Kifua Kikuu kutoka watu 948 mwaka 2017” Alisema

 

Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Said Khamis Ahmada, akiwasilisha Mada juu ya maradhi ya Kifua Kikuu.


Kwa upande wake, mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma kanda ya Pemba Hamad Omar Hamad, amesema  takwimu zionanesha jumla ya Wazanzibari 7,524 na virusi vya Ukimwi kwa mwaka 2019, ambapo idadi ya maambukizi jumla katika jamii ni sawa na asilimia 0.4.

 

Ameongeza kuwa, kwa mujibu wa takwimu wanawake ndio wanaoongoza kwa maambukizi ya virusi vya Ukimwi Kuliko wanaume Visiwani Zanzibar. 

 

“Wagonjwa 3 wa mwanzo walioambukizwa virusi vya Ukimwi Zanzibar waligunduliwa mwaka 1986, katika hospiati ya Mnazi Mmoja, takwimu zinaonesha idadi ya maambukizi kwenye jamii ni asilimia 0.4 hadi sasa ambapo jumla ya watu 7524 wameambukizwa VVU mwaka 2019 huku takwimu zikionesha wanawake kuwa wengi ikilinganishwa na wanaume katika maambukizi hayo” Hamad Omar Hamad


Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma kanda ya Pemba Hamad Omar Hamad, akiwasilisha Mada juu ya maambukizi ya maradhi ya Uviko19 na Ukimwi.


Abdi Suleimani ni mwandishi wa gazeti la Zanzibar leo Kisiwani Pemba, amewaomba watendaji wa wizara ya afya kisiwani Pemba kuandaa program maalumu za kutoa mafunzo kwa vijana hususan bodaboda ili kuwanusuru vijana hao.

 

“Licha ya mafunzo haya kwa waandishi wa habari lakini bado muna jukumu kubwa la kuendelea kutoa elimu kwa vijana hususan vijana wa bodboda wa Machomanne wameharibika sana kimaadili na inadaiwa kuwa kuna baadhi ya ndugu zetu wanatoka Tanzania bara kuja Pemba kwa ajili ya kufanya biashara ya kuuza miili yao na inasemekana wateja wao wakubwa ni vijana hususan bodaboda sasa musipoliangalia hili kwa macho mawili tunaweza kuja kuwapoteza vijana wengi sana hapo baadae” Abdi Suleiman

 

Wa Pili kutoka kulia ni Mwandishi wa Habari wa Gazeti la Zanzibar Kisiwani Pemba Leo Abdi Suleiman akiwa na Mwandishi mwenzake Habiba Zarali Rukuni.


Akiitoalea ufafanuzi hoja hiyo, Mratibu wa Kitengo Shirikishi ZIHHTLP Pemba, Khamis Hamad Ali, amesema Wizara ya Afya Zanzibar imeandaa utaratibu wa kukutana na wananchi mbali mbali wakiwemo Vijana ili kutoa elimu juu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi ikiwemo namna ya kujikinga na maambukizi sambamba na kupima afya zao kwa hiari.

 

“Kwanza ahsante sana kwa taarifa pili niseme kuwa Wizara ya Afya Zanzibar tumekuwa na utaratibu endelevu wa kukutana na wananchi mbali mbali wakiwemo Vijana katika kutoa elimu ya kujikinga maambukizi ya VVU pamoja na kupima afya zao kwa hiari na ukweli ni kwamba vijana wengi sasa hivi wana taaluma ya kutosha kuhusu VVU na kutambua umuhimu wa kucheki afya zao mara kwa mara” Mratibu ZIHHTLP


Mratibu wa Kitengo Shirikishi ZIHHTLP Pemba, Khamis Hamad Ali.

Nao Waandishi walioshiriki katika hafla hiyo wameahidi kuyafanyia kazi mafunzo hayo kwa kuandika habari zitakazo waelimisha wananchi kuhusu athari hasi za kuwanyanyapaa wahisiwa wa maradhi ya kuambukiza ikiwemo Kifua Kikuu, Uviko19 pamoja Ukimwi.

 

Baadhi ya Waandishi wa Habari Kisiwani Pemba walioshiriki katika Mafunzo hayo.


Mafunzo hayo ya siku moja yalikuwa na lengo la kutoa elimu kwa waandishi wa habari Kisiwani Pemba juu ya athari ya kuwanyanyapaa wahisiwa wa maradhi ya kuambukiza ikiwemo Kifua Kikuu, Uviko19 pamoja na Ukimwi.



Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Said Khamis Ahmada.

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 

 




#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top