Mkuu wa wilaya ya Makete Juma Sweda amesema kuwa kitendo cha baadhi ya wanaume wa kata ya Lupalilo kutaka kwenda na wake zao kuzima moto unapojitokeza wakati wao wapo, ni kitendo cha aibu ambacho hajawahi kukiona sehemu yoyote
Sweda ameyasema hayo Oktoba 10, 2022 wakati wa uzinduzi wa kamati za usimamizi wa matumizi bora ya moto kwa wilaya ya Makete uliofanyika katika kijiji cha Mago kata ya Lupalilo wilayani Makete baada ya kutoa maelekezo kuwa moto unapojitokeza wanaume pekee ndio waende kuuzima huku akijionea wanaume wanapinga utaratibu huo hadharani
Baada ya kuona wanaume bado wanaendelea kuupinga utaratibu huo, mkuu huyo wa wilaya alilazimika kutoa onyo akisema kuwa ole wake mwanaume atakayejifungia ndani kama moto umetokea kwenye kijiji chake na kuwataka wanawake wabaki majumbani kwa ajili ya uangalizi wa watoto.
Kadhalika mkuu huyo wa wilaya ameonya tabia ya baadhi ya wanaume kuwatelekezea wanawake majukumu na wao kukimbilia kulewa akisema kuwa atahakikisha analifuatilia jambo hilo ili kila mmoja asimame kwenye nafasi yake
Badhi ya wanawake wamesema kuwa ujio wa mkuu wa wilaya katika kijiji hicho umekuwa faraja kwao kwani yote aliyosema ni ya kweli hivyo utakapotokea moto wanaume wawajibike kwenda kuuzima.
Baada ya kumalizika kwa mkutano huo baadhi ya wanaume wamezungumza na Green fm kuhusu agizo la mkuu huyo wa wilaya la kwenda kuzima moto pasipo kuwa na wanawake.