Mkuu wa mkoa wa Njombe @anthony_mtaka ametoa siku 10 kwa bodi ya kiwanda cha maziwa kukutana na wadau wote wa maziwa ili kutangaza mipango ya kumtafuta mwekezaji mpya atakayekinusuru kiwanda hicho kupigwa mnada baada ya kushindwa kujiendesha.
Aidha Benki ya Kilimo TADB inatarajia kupiga mnada kiwanda hicho hapo disemba mwaka huu kutokana na kushindwa kufanya marejesho ya mkopo wa Bilioni 1.6 kwa mwaka mzima sasa waliopewa wamiliki wa kiwanda hicho ili kiweze kujiendesha kwa maslahi mapana ya wafugaji.
Awali mwenyekiti wa Halmshauri ya wilaya ya Njombe Valentino Hongoli na Filoteus Mligo makamu mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Njombe ambao ni wanahisa wamesema kwa kuwa hisa zao ziliwekwa kisheria ni lazima wanahisa wakutane na mabaraza ya madiwani yakajadili suala hilo huku Padre Athanas Mgimba kwa niaba ya Kanisa Katholiki ambalo nalo linamiliki hisa akisema walianza mchakato wa kutafuta mwekezaji mwingine.
Katika kikao hicho mkuu wa mkoa Antony Mtaka amesema mkwamo wa kiwanda hicho unatokana na kumilikiwa na watu wengi ambapo amezitaka Halmshauri za Njombe mji,Njombe Wilaya na Kanisa Katholiki kuchukua hisa zao zenye thamani ya milioni 9.5 kila mmoja ili wabaki wafugaji ambao watamweka mwekezaji mwenye uwezo.
Mbunge wa jimbo la Njombe mjini Deo Mwanyika na Deo Sanga mbunge wa Makambako Wamekiri kupokea malalamiko mengi toka kwa wafugaji katika maeneo wanayofanya mikutano yao juu ya madai ya fedha zao za maziwa kiwandani hapo.
Baadhi ya wafugaji akiwemo Remigius Mtewele na Agness Wella wamesema hawako tayari kuendelea kuwabeba wanahisa ambao hawasaidii kuboreshwa kiwanda wala kuwapigania kulipwa fedha zao za maziwa.
Disemba mwaka huu Benki ya kilimo TADB inatarajia kupiga mnada kiwanda hicho ambacho kimekuwa kikidaiwa fedha nyingi na benki pamoja na wafugaji kutokana na kujiendesha kwa hasara