Mfanyabiashara mmoja jijini Mbeya aitwaye Amosi Daudi (52) amefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kumuingilia kinyume cha maumbile mtoto wa kiume (09) katika eneo la Ilemi jijini humo.
Akisoma maelezo ya hati ya mashtaka kwenye kesi hiyo mbele ya hakimu anayesikiliza kesi hiyo Sangiwa Mtengeti, mwendesha mashtaka wa serikali wakili Rosemary Mgenyi akishirikiana na wakili mwenzake Davice Msanga amesema mtuhumiwa Amosi Daudi ambaye ni mfanyabiashara mkazi wa Ilemi alitenda kosa hilo katika tarehe tofauti kati ya Januari 2022 na Oktoba 2022 katika eneo la Ilemi jijini Mbeya.
Wakili Rosemary Mgenyi amesema mtu huyo akiwa na ufahamu timamu alimwingilia kinyume cha maumbile mtoto (Jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka tisa kitendo ambacho ni kinyume na kifungu namba 154 (1) a na 154 (2) cha sheria ya kanuni za adhabu sura ya 16 kilichofanyiwa marekebisho mwaka huu 2022.
Mshtakiwa huyo amekana kutenda kosa hilo huku akiwa anawakilishwa na mawakili wawili mahakamani hapo.
Kwa mazingira hayo upande wa mashtaka unalazimika kuwasilisha ushahidi na vieleelezo vyake mbele ya mahakama ili kuthibitisha madai yake hayo dhidi ya mfanyabiashara huyo kuelezwa kumnajisi mtoto wa kiume kwa kumwingilia kinyume cha maumbile.
Hakimu mkazi katika mahakama ya hakimu mkazi Mbeya Sangiwa Mtengeti ameahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 17 kwa ajili ya kusoma maelezo ya awali namna mshtakiwa alivyotekeleza tukio hilo ambalo analikana kisha shauri hilo kuanza kusikilizwa na mshtakiwa amepata dhamana hadi baadaye juma lijalo.