Jumuiya ya waalimu wa madrasa Pemba (JUMWAMPE) imewataka viongozi wa Shehia wa jumuiya hiyo pamoja na waalimu wa madrasa kuunga mkono juhudi za maendeleo zinazofanywa na jumuiya hiyo ili kuboresha maslahi ya waalimu wa madrasa kisiwani Pemba.
Mapema akizungumza na viongozi wa jumuiya hiyo kutoka Wilaya mbili za Chake Chake na Mkoani huko katika Msikiti wa Mtambile Polisi, katibu wa jumuiya hiyo Sheikh Omar Othman Nassor, amesema jumuiya hiyo inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo ikiwemo uhaba wa vitendea kazi, ofisi pamoja na rasilimali fedha.
"Kama tunavyofahamu kama jumuiya tunalazimika kila baada ya miaka mitatu tunatakiwa kufanya Mkutano mkuu na ukifanya mahesabu ya haraka haraka kuanzia kukodi ukumbi na chakula kwa ajili ya washiriki tunatakiwa kuwa na kiasi cha shilingi milioni nne, ni ukweli ni kwamba kiasi hicho cha fedha hadi sasa hatuna tunafanyaje" Alihoji
"Lakini pia ili jumuiya iweze kusonga mbele na kufanya kazi zake ipaswavyo tunatakiwa kuwa na vifaa vya kisasa ikiwemo komputa, mashine ya kuchapa na kutoa nakala ngumu (Printers) kuwa tovuti (Website) mitando ya kijamii kwa ajili ya kuchapisha taarifa zetu ili watu waone yale tunayoyafanya na vitu vyote hivyo vinahitaji rasilimali fedha, kwahivyo hatuna budi kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha tunafanikisha kupata vitu hivyo" Katibu Jumwampe.
Aidha ameongeza kuwa miongoni mwa changamoto zinazowakabili wa walimu wa madrasa ni pamoja na hali duni za kimaisha sambamba na wanafunzi kudharau masomo ya dini na badala yake kutumia muda mwingi katika elimu ya dunia ikiwemo kwenda twisheni.
"Suala la twisheni limekuwa ni tatizo kubwa kwetu, kwasababu wanafunzi wanatumia muda mwingi kusoma masomo ya Shule kuliko masomo ya dini, ukiacha muda wa Serikali lakini wanatumia muda wa ziada kwenda twisheni kiasi kwamba sisi wa elimu ya dini hatuwapati hata kidogo hili ni tatizo na muda umefika sasa kukaa chini na Wizara ya elimu kufanya majadiliano juu ya suala hili" Alisema
Nao baadhi ya viongozi hao wamesema, muda umefika wa kukutana maafisa wa elimu wa kila Wilaya ili kujadili suala la twisheni kwa wanafunzi ili kila upande uweze kufaidika na wanafunzi hao.
"Unamkuta mwanafunzi kutoka Jumatatu hadi Jumapili anakwenda skuli na akirudi Skuli anakwenda twisheni, sasa sisi waalimu wa elimu ya dini tunawakosa badala yake tunabaki na wale wadogo wadogo, sasa kwakweli suala hili linaturudisha nyuma sana" Alisema mmoja miongoni mwa viongozi hao.
Mkutano huo wa siku mbili uliyowashirikisha viongozi wa jumuiya hiyo ngazi za Shehia kutoka Wilaya ya Chake Chake na Mkoani ulikuwa na malengo mbali mbali ikiwemo kujadili maendeleo ya jumuiya, kuwajenga walimu katika misingi bora ya utekelezaji wa majukumu yao sambamba na kujadili suala la mkutano mkuu wa jumuiya hiyo ambao unatarajiwa kufanyika December 11.2022.