Jeshi la Polisi Mkoa wa Njombe linamshikilia mkazi wa Kata ya Kihesa mkoani Iringa, Baraka Mtewe (30) kwa tuhuma za mauaji ya aliyekuwa mke wake Jackline Nyondo (27).
Hayo yamesemwa Oktoba 31, 2022 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Hamis Issah wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema kabla ya kifo Jackline alikwenda Makambako kumsalimia mumewe lakini katika sintofahamu iliyotokea mumewe huyo alichukua kitu kizito na kumpiga nacho na hatimaye alipoteza maisha.
Kamanda Issah amesema baada ya kufanya tukio hilo mtuhumiwa alichukua mashuka na vitu vingine kisha kumfunika marehemu na baadae alifunga mlango na kutoweka pasipo julikana.
Alisema takribani mwaka mmoja na nusu tangu mtuhumiwa huyo afanye tukio hilo lakini sasa amekamatwa akiwa amejificha kwa mama yake mzazi mkoani Iringa.
"Mwanaume huyu alichukua mashuka na vitu vingi na kumfunika baadaye akafunga mlango kwa nje na kutoweka kusikojulikana kwa muda wa mwaka mmoja na nusu" amesema Issah.
Amewataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani mkono wa serikali ni mrefu na yeyote atakaye fanya uhalifu atakamatwa.