Mchunga Mifugo ya Marwa Kera mkazi wa Nyichoka Wilaya ya Serengeti anatuhumiwa kumuua Weisiko Nyangi (37)mke wa bosi wake na mwili kuutupa porini kisha kuiba ng'ombe 5 na kupeleka mnadani.
Afisa mtendaji wa kijiji cha Nyichoka Itabe Nkiri leo Alhamisi Januari 12,2023 ameitaarifu Serengeti Media Centre kuwa tukio la mauaji linadaiwa kutokea Januari 10 majira ya saa 5 asubuhi.
Amesema,mtuhumiwa ambaye ni mkazi wa kitongoji cha Songambele jina limehifadhiwa anadaiwa kumkata huyo mwanamke shingo kwa nyuma kwa kutumia panga na kubakiza koromeo kisha akamfunika na matawi ya miti.
Amesema,januari 12 wananchi wameendesha msako na saa moja asubuhi wamefanikiwa kuupata mwili ukiwa kichakani umefunikwa matawi ukiwa umeishashambuliwa na fisi.
Emmanuel Nyangaka mkazi wa Kitongoji hicho ameambia Serengeti Media Centre kwa njia ya simu kuwa,"siku ya tukio mme wa huyo mama alikuwa safari,huyo mtuhumiwa saa 5 asubuhi alirudi nyumbani bila mifugo na kumwambia huyo mama kuwa ng'ombe mmoja amenaswa na waya wa majangili hivyo akamsaidie kumnasua,"amesema.
Amesema,walipokaribia eneo la kichaka huyo mama akiwa ametangulia akamkata shingo kwa nyuma na kubakiza koromeo kisha akamwingiza kichakani na kufunika mwili kwa matawi ya miti
"Baada ya mauaji akarudi akalala hapo na asubuhi jana akawaambia watoto wa bosi wake kuwa mzee amesema waandae ng'ombe tano wapeleke mnadani,zikaandaliwa na akapeleka bila wasiwasi"amesema.
Na kuwa wakati anaenda mnadani majirani ambao walijua Kera amesafiri walimpigia simu kumuuliza kama ndiye kamtuma,"ilibidi atoke Tarime awahi mnadani Mugumu na kumkuta akisaka soko la mifugo yake akamkamata na kumfikisha polisi,wakati huo hajajua kama ndiye kahusika na mauaji ya mke wake,"amesema na kuongeza,
"Kwa kuwa ilikuwa siku ya pili mke wake hajaonekana ilibidi ipigwe yowe wananchi tukaanza msako na kuupata ukiwa mkono na mguu umeishashambuliwa na fisi"amesema.
Mwili wa marehemu umesafirishwa kwenda kijiji cha Nyang'arang'a Mugeta kwa ajili ya maziko na mtuhumiwa anashikiliwa na Polisi Mugumu.