WAANDISHI WASHAURI SHERIA NO. 4\2005 KUFANYIWA MAREKEBISHO, KUPAMBANA NA UDHALILISHAJI ZANZIBAR.

Hassan Msellem
0

Mapambano dhidi ya vitendo vya udhalilishaji yamekuwa yakikabiliwa na changamoto kadhaa, miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na sheria ambazo zinaonekana kuwa na mapungufu mbali mbali katika utekelezaji wake.


Sheria nambari 4 ya mwaka 2005 ya kulinda wari na watoto waliozaliwa na mzazi mmoja pamoja na kutoa tafsiri halisi ya mwari, ni miongoni mwa sheria yenye kasoro kadhaa ikiwemo tafsiri halisi ya mwari, kuwaruhusu vijana kufanya mapenzi nje ya ndoa kwa sharti la mwanamke kutokupata ujauzito, hukumu Kwa upande wa mwanamke kuwa ndogo na wengine kusema ni hukumu kandamizi dhidi ya wanawake pamoja na adhabu kuwa ndogo kwa upande wa mwanamme.

 

kwa mujibu wa tafsiri ya sheria hiyo mwari maana yake ni mwanamke ambae hajaolewa na ambae mwenye umri wa miaka 18 mpaka 21 na ambae hajazaa.

 

Hukumu ya kosa la kumpa ujauzito mwari Kifungu cha 3 (3) kimeeleza kuwa “aliyempa mimba mwari, atumikie chuo cha mafunzo kwa muda usiozidi miaka 3 na usiopungua miaka 5.


Kifungu 3 (6) mwari aliyepewa mimba atatumikia jamii kwa kipindi cha miezi 6 kuanzia miezi mitatu baada ya kujifungua.

 

WANANCHI WANASEMAJE KUHUSU SHERIA HII?


Idawaonline.com imezungumza na wananchi mbali mbali kuhusu sheria hii, ambapo baadhi ya wananchi wamesema mapungufu katika sheria hiyo ni kutofautiana kwa adhabu kati ya mwanamme na mwanamke jambo ambalo sio sahihi kwa vile wote ni watu wazima na wamefanya tendo la ndoa kwa makubaliano.

 

Juma Said Khatib miaka 48 mkaazi wa Shehia ya Wara, amesema kutofautiana na kwa adhabu kunapelekea kuongezeka kwa vitendo vya hivyo kwani adhabu hizo haziwafanyi wanawake kupata mabadiliko ya kitabia.

 

“Binafsi sikubaliani na Sheria hiyo ya adhabu kwasababu kama mwanamke ni mtu mzima kisheria hajalishi kama amewahi kuolewa ama laa sheria inatakiwa kutoa adhabu sawa kwa upande wa mwanamme na mwanamke endapo wamekubaliana” alisema


 WANAHARAKATI.


Kwa upande wa wanaharakati wa kupinga vitendo vya udhalilishaji Kisiwani Pemba, wamesema adhabu ya kutumikia kifungo miaka 3 na usiopungua miaka 5 ni ndogo hali inayopelekea kuongezeka kwa matukio ya udhalilishaji.

 

“Kwakweli adhabu katika Sheria hii bado ni ndogo sana maana ukiangalia miaka mitatu hadi mitano kwa kupoteza heshima na thamani ya mtu ukizingatia katika karne hii miaka inakwenda speed sana, kwahivyo sisi kama wanaharakati wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji tunapendekeza sheria hii ifanyiwe mabadiliko ili kuhakikisha watoto wakike na wanawake wanatimiza ndoto” alishauri

 

Mkurugenzi wa jumuiya Tumaini Jipya Pemba(TUJIPE) Tatu Abdalla Msellem, ameshauri kuondolewa kwa adhabu ya miezi sita kwa upande wa wanawake kwani kuwepo kwa adhabu hiyo inazidi kuwakandamiza wanawake ambao wanaopewa ujauzito ikizingatiwa kuwa wanawake wanaojifungua nje ya ndoa wanapitia wakati mgumu wa matunzo yake pamoja na mtoto.

 

“Mimi nadhani kuwepo kwa sheria ya adhabu ya miezi sita kwa wanawake wanaojifungua nje ya ndoa ni sheria inayozidi kuwaongezea maumivu na fedheha wanawake kwani inawapa nafasi wanaume kuendelea kuwadhalilisha wanawake” alisema

 

Mratibu wa Chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania (TAMWA) Kisiwani Pemba Fat-hiya Mussa Said, amesema upo wa Sheria za udhalilishaji zenye mapungufu zinapelekea kukwamisha juhudi za mapambano dhidi ya vitendo hivyo.

Aidha, mratibu huyo ameviomba vyombo vya habari kuongeza nguvu katika kuandika habari na Makala mbali mbali zinazoshikiza kufanyiwa marekebisho Sheria hizo.

 

“Vitendo vya udhalilishaji limekuwa ni janga kwa taifa kiasi kwamba kila siku tunaposikiliza vyombo vya habari tunasikia taarifa kuhusu vitendo hivyo, hivyo basi zile sheria zote ambazo zinaonekana kurudisha nyuma juhudi dhidi ya mapambano ya vitendo vya udhalilishaji zinapaswa kufanyiwa marekebisho haraka iwezekenavyo” Mratibu Tamwa Pemba.


WAANDISHI WA HABARI

 

Waandishi wa habari nao ni wadau wakubwa katika kuzifanyia uchechemuzi sheria za udhalilishaji ambazo zinaonekana kuwa na mapungufu mbali mbali katika utekelezaji wake.

 

Waandishi wa habari nao wamesema sheria namba 4 ya mwaka 2005 ya kulinda wari na watoto waliozaliwa na mzazi mmoja ni sheria inayokinzana na misingi ya dini, mila na desturi za wazanzibari kwa kutokuwatia hatiani watu wanaofanya mapenzi nje ya ndoa endapo kama mwanamke hakupata ujauzito, hivyo wameomba kufanyiwa marekebisho kwa sheria hiyo na badala yake kutendo cha kufanya mapenzi nje ya ndoa iwe ni kosa hata kama mwanamke hatopata ujauzito.

 

“Binafsi nikiwa kama mtetezi wa jamii sikubaliani na sheria hii kwasababu asilimia 99 ya Wazanzibari ni waumini wa dini ya Kiislamu pamoja na dini ya Kikristo mila na desturi ambazo zote hazikubaliani na tabia ya kufanya mapenzi nje ya ndoa, kwahivyo naomba sana sheria hii ibadilishwe badala ya kwamba kufanya mapenzi nje ya ndoa iwe ni kosa kisheria kama ilivyo kwenye dini hata kama mwanamke hakupata ujauzito” Salum Ali Msellem, mwandishi wa radio Istiqama Pemba

 

Suala la usawa wa adhabu ni miongoni mwa nukta ambazo zimegusiwa katika sheria hiyo, ambapo mwandishi wa habari wa ZBC Pemba Hadija Kombo Khamis, amependekeza wanawake kupewa adhabu sawa na ile wanayopewa wanaume kwani kuwepo kwa utofauti wa adhabu kunachangia kwa kiasi kikubwa kukoma kwa vitendo vya udhalilishaji.

 

“Mimi nadhani suala la kutofautiana kwa adhabu ni suala linalohitaji marekebisho kwasababu haiwezekani mwanamke mtu ambaye anafahamu kuwa kufanya mapenzi nje ya ndoa ni kosa kisha baada ya kupata ujauzito mwanamme apewe adhabu kali na mwanamke apewe adhabu nyepesi hii sio sahihi kabisa kwani juhudi za kutokomeza vitendo vya udhalilishaji haitozaa matunda” HADIJA KOMBO ZBC

 

MAHAKAMA

 

Kwa mujibu wa mwendesha mashtaka wa Serikali kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar Ali Amour Makame, amesema sheria namabri 4 ya mwaka 2005 ni miongoni mwa Sheria zinazolalamikiwa kuwa na mapungufu kutokana kukinzana na dini, mila na desturi za Wazanzibari katika kupambana na vitendo vya udhalilishaji.

 

“Ni kweli kwamba Sheria hii ina mapungu kadhaa ikiwemo kutofautiana kwa adhabu baina ya mwanamme na mwanamke jambo ambalo wanasema sio sahihi lakini pia suala la kufanya mapenzi kutokuwa ni kosa na badala yake baada ya mwanamke kupata ujauzito pekee kuonekana ndio ni kosa” alisema

Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar Ali Amour Makame.


MAONI YA MHARIRI.

Ni matumaini ya mhariri wa Makala hii kuwa endapo Sheria hii itafanyiwa marekebisho itaondosha malalamiko ya wananchi sambamba kuwarahishia kazi wanaharakati wanaopambana dhidi ya vitendo vya udhalilishaji visiwani Zanzibar.

 

Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 

 

#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top