Mfanyabiashara Aman Elikana (38) aliyekuwa anakabiliwa na kesi ya mauaji, ameachiwa huru na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, baada ya upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yake.
Elikana alikuwa akituhumiwa kumuua askari Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani, mwenye namba D8254 Sajenti Mensah kwa kumpiga risasi kifuani iliyomvunja mbavu upande wa kulia na kutoboa mapafu.
Ilidaiwa kuwa mauaji hayo yalifanyika katika mataa ya kuongozea magari eneo la Sayansi, Kijitonyama.
Uamuzi wa kumwachia huru umetolewa Jumatatu Machi 20, 2023 na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Romuli Mbuya, wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya kutolewa hukumu.
"Upande wa mashtaka imeshindwa kuthibitisha mashtaka dhidi ya mshtakiwa huyo, hivyo mahakama ina muachia huru Aman," amesema Hakimu Mbuya.