Mzee mwenye umri wa miaka 73 amefariki dunia huku wengine 365 wakilazwa hospitalini baada ya kula nyama ya ng'ombe anayeshukiwa kuugua ugonjwa wa kimeta.
Wakazi hao wa kijiji cha Gatumbi eneo la Iriari, kaunti ndogo ya Runyenjes, kaunti ya Embu, wanadaiwa kula nyama hiyo wiki jana.
Kwa mujibu wa ripoti ya idara ya afya ya kaunti ya Embu, Patrick Ndwiga Njagi alifariki Jumapili, Machi 18, siku moja baada ya kulazwa katika Hospitali ya Runyenjes Level 4 na baadaye hospitali ya Embu Level 5 akiwa na dalili za ugonjwa wa kimeta.
Marehemu anasemekana kuanza kuonyesha dalili za ugonjwa wa kimeta baada ya kusaidia majirani zake kumchinja mnyama huyo ambaye baadaye aliuzwa kwa mamia ya wakazi.
"Mnamo tarehe 16 Machi mgonjwa alionyesha dalili za kutapika, kushindwa kupumua, kutetemeka na vidonda kwenye mikono yote miwili," "Jumamosi tarehe 18 Machi 2023 alilazwa katika hospitali ya Runyenjes Level 4 ambako alihamishiwa hadi Hospitali ya Embu Level 5 jioni ya siku hiyo hiyo.
Mgonjwa alifariki tarehe 19 Machi saa 12.00 mchana," ilisema taarifa ya idara hiyo na kuongeza kuwa kaunti hiyo imechukua tahadhari kuhusu mkurupuko wa ugonjwa huo katika kaunti ndogo ya Runyenjes.
Jumla ya watu 365 walipimwa na kutibiwa katika hospitali moja na sasa hali zao zinaendelea vizuri.
idara hiyo ya afya ilisema kuwa takriban watu 1,000 wanashukiwa kula nyama hiyo ambayo ilinunuliwa na angalau familia 200.
Kufuatia kisa hicho, polisi na maafisa wa afya ya umma kutoka kaunti hiyo sasa wanamsaka mshukiwa anayeaminika kukagua nyama hiyo licha ya kukosa stabadhi mwafaka.