UBAKAJI: ZIMWI LINALOKATISHA NDOTO ZA WATOTO WA KIKE ZANZIBAR.

Hassan Msellem
0

Na, Hassan Msellem-Pemba

Alikuwa miongoni mwa wazazi waliokuwa na matumaini makubwa ya kuwa siku moja mtoto wake angemaliza shule na kupata kazi ya ndoto yake.


Hata wakati akiendelea kufanya uwekezaji ikiwemo kumpatia mahitaji yote ya shule akiwa kidato cha kwanza, mtoto wake alikatisha masomo na kuacha shule.

 

Idrissa Bai Pandu (58), mkaazi wa Chambani Wilaya ya Chake Chake Mkoa wa Kusini Pemba anasema mtoto wake amekatisha masomo baada ya kubakwa, kitendo kilichomuachia majeraha makubwa ya kisaikolojia.

 

“Mwanangu alikuwa ana ufahamu mzuri tu na alikuwa anapenda kusoma na alikuwa ana ndoto nyingi sana ikiwemo kuwa mwanasheria lakini ndoto hizo zote zimepotea kutokana na kushindwa kuendelea na masomo baada ya kubakwa kwa nguvu,” anasema kwa uchungu.

Mara baada ya binti yake kubakwa, Pandu anasema aliathirika kisaikolojia mpaka kufikia hatua ya kupata matatizo ya akili na kusababisha ashindwe kuendelea na masomo.

 

“Kitendo alichofanyiwa kilimfanya kila anapokutana na watu wengi kujisikia vibaya na kuwa kama mtu aliyechanganyikiwa,” anasema huyo, ambaye matumaini kwa binti yake kuendelea na masomo anaona kama yamefifia.

 

Mzee huyo ni miongoni mwa baadhi ya wazazi visiwani Zanzibar ambao wamekuwa wakikosa usingizi na kutafuta kila njia ya kuwalinda watoto wao ili wasitumbukie kwenye mikono ya watu wabaya wakiwemo wabakaji na kutimiza ndoto zao.

 

Hata hivyo, juhudi hizo siyo wakati huzaa matunda.

 

“Mimi kama kiongozi wa familia nafahamu vyema sana jukumu la kuhakikisha nawalea watoto wangu katika maadili mema ili kuwalinda dhidi ya vitendo vya ubakwaji lakini unajua kuna mambo mengi sana yanayosababisha kutokea kwa vitendo hivyo,”anasema Ali Omar Juma, mkazi wa Chake Chake.

 

“Miongoni mwa hivyo ni marafiki wabaya, matumizi mabaya ya simu pamoja na vishawishi ukiachana na wale ambao wanabakwa kwa kutumia nguvu,” anasema Juma

(67).

 

Juma, baba wa watoto anasema licha ya wazazi kutimiza wajibu wao, mazingira wanayokuwepo watoto nje ya nyumbani huchangia kufanyiwa ukatili wa kijinsia ikiwemo ubakaji kwa watoto wa kike.

 

Ubakaji umekuwa ukihusishwa pia na imani za kishirikina, ukosefu wa maadili na kushamiri kwa makundi rika yanayochochewa na matumizi ya dawa za kulevya.

 

Hata hivyo, Sheria ya Watoto ya Zanzibar ya mwaka 2011 inasisitiza jamii na wazazi wazazi na jamii kubeba jukumu la kumlinda na kila hatari ikiwemo vitendo vya uzalilishaji vinavyorudisha nyuma ustawi na ukuaji wake.

 

HALI ILIVYO ZANZIBAR.

 

Kwa mujibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Tawi la Pemba na Jumuiya ya Tumaini Jipya Pemba (TUJIPE), matukio 88 ya ubakaji yaliripotiwa mwaka 2022 kutoka 44 ya mwaka juzi

Chake Chake.

 

Hiyo ni sawa na kusema ndani ya kipindi cha mwaka mmoja, matukio ya ubakaji yaliongezeka kwa asilimia 50, kasi ambayo ni kubwa hasa kwa mstakabali wa mtoto wa kike.

 

Tatizo la ubakaji siyo la Chake Chake pekee, bali linasumbua katika maeneo mengine ya Zanzibar.

Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar (OCGS) inaeleza kuwa matukio ya ubakaji Zanzibar yameongezeka kutoka matukio 1,222 mwaka 2021 hadi matukio 1,360 mwaka 2022.

 

Hilo ni ongezeko la matukio 138 (asilimia 11.3) ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.

 

Katika kupambana na vitendo vya ubakaji nchini viongozi wa dini nao wanajukumu kubwa la kuhakikisha vitendo hivyo vitokomezwa.

 

Lakini je, wanafahamu dhima na wajibu wao katika jamii katika kuielimisha jamii ili kukabiliana na vitendo vya ubakaji?

 

Naibu Katibu kutoka Ofisi ya Mufti Mkuu kisiwani Pemba, Sheikh Said Ahmad Mohammed anasema wamekuwa na utaratibu wa kutoa mafunzo juu ya vitendo vya ubakiji kwa walimu wa madrasa kila baada ya miezi mitatu ili kuhakikisha wanapata elimu hiyo kusudi waweze kuitoa kwa wanafunzi.

 

Pia wana programu za kutoa elimu ya kupambana na vitendo vya ubakaji kwa wananchi katika maeneo wanayoishi pamoja na vyombo vya habari.

 

“Kiujumla Ofisi ya Mufti Kisiwani Pemba imeandaa programu nyingi sana katika kupambana na vitendo vya ubakaji, miongoni mwa program hizo ni kutoa mafunzo kwa walimu wa madrasa, kupita mitaani pamoja na kutumia vyombo vya habari kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kutosha kupambana na vitendo vya ubakaji,” anasema Sheikh Mohammed.

 

Licha ya walimu wa madrasa kutakiwa kuwa mfano wa kuigwa, baadhi yao wamekuwa wakishiriki vitendo hivyo kikatili kwa watoto wa kike.

 

Kwa mujibu wa Ofisi ya Mufti Mkuu Kisiwani Pemba, walimu wa madrasa saba wametuhumiwa kwa vitendo vya ubakaji mwaka 2022, ambapo walimu 3 kati ya hao walikutwa na hatia na kuhukumiwa kutumikia vifungo mbalimbali.

MAHAKAMA NAYO YATIMIZA WAJIBU WAKE.

Kwa mujibu wa Ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali Mkoa wa Kusini Pemba, kesi 128 za ubakaji zilifikishwa Mahakama ya Mkoa Chake Chake mwaka jana. Kati ya kesi hizo, 97 zilitolewa hukumu na kesi 56 washtakiwa walikutwa na hatia na kuhukumiwa kutumikia vifungo pamoja na kulipa fidia.

 

“Kwa mujibu wa takwimu tulizonazo ukiangalia mwaka 2022 idadi ya matukio ya ubakaji kwa wanafunzi yamekuwa mengi zaidi kuliko mwaka 2021, ambapo takwimu zetu zinaonyesha takriban kesi 128 ziliripotiwa katika mahakama yetu ikilinganisha na mwaka jana ambapo kulikuwa na kesi 88,

 

“Hivyo hii inadhihirisha kuwa bado suala la ubakaji ni donda ndugu katika visiwa vyetu vya Zanzibar licha ya Mheshimiwa Rais wa Zanzibar kuanzisha mahakama maalum ya kupambana na makosa udhalilishaji,” anasema Mwendesha Mashtaka wa Serikali Ali Amour Makame.

Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Pemba, Fat-hia Mussa Said suala la ubakaji siyo la kufumbiwa macho na kila mtu anawajibika kukabiliana nalo.

 

“Sisi kama wanaharakati wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji ikiwemo ubakaji tumekuwa tukifanya programu mbalimbali ikiwemo kukutana na wadau, waandishi wa habari, walimu wa madrasa, viongozi wa dini, vipeperushi, kampeni mbalimbali, makongamano na mijadala ili kuhakikisha wananchi wanapata uelewa katika

kukabiliana na vitendo hivyo.

 

“Kwa kiasi fulani tunasema tumepiga hatua kwa sababu licha ya kuona matukio ya ubakaji yameongezeka lakini hiyo imetokana na wanachi kutoa taarifa pindi yanapotokea matukio ya ubakaji sambamba na vyombo vya habari kuripoti matukio hayo,” anasema Fat-hia.



Tags

Post a Comment

0 Comments
* Please Don't Spam Here. All the Comments are Reviewed by Admin.
Post a Comment (0)

 


 

 




#buttons=(Accept !) #days=(20)

Our website uses cookies to enhance your experience. Learn More
Accept !
To Top