Jeshi la Polisi mkoani Njombe limetangaza kumkamata mtu mmoja anayetuhumiwa kuhusika kuchoma maduka ya Jumuiya ya wanawake wa CCM UWT Wilaya ya Njombe hapo April 1 mwaka huu akiwa na lengo la kutaka kujipatia faida kupitia bima ya biashara yake.
Akizungumza na vyombo vya habari Kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe Hamis Issah amesema mtu huyo ambaye jina lake limehifadhiwa kwa sababu za kiuchunguzi alitekeleza tukio hilo baada ya kuhamisha biashara yake lengo likiwa ni kutaka kunufaika na bima aliyokuwa analipia.
Sanjari na hilo lakini pia Kamanda Issah amethibitisha kutokea kwa vitendo vya ukiukwaji wa maadili vinavyodaiwa kufanywa na baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari Yakobi kujihusisha na mapenzi ya Jinsia moja na kwamba hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa.
Baaadhi ya wakazi wa Njombe akiwemo Joyce Chumi wamesema serikali inapaswa kutoa tamko ambalo wananchi watalifuata juu ya vitendo hivyo vya ushoga.
Kwa upande wao baadhi ya wanafunzi wa TYCS wakiwa kwenye moja ya Kongamano mkoani Njombe wanakiri kuwapo kwa mmomonyoko wa maadili kwa baadhi ya vijana jambo ambalo kazi ya ziada inapaswa kufanyika na viongozi wa dini na serikali.
Hata hivyo Jeshi la Polisi limeendelea kufanya misako mbalimbali na kufanikiwa kukamata mali mbalimbali za wizi zikiwemo kompyuta,Maharage,Mbolea pamoja na Matairi Matatu ya Magari makubwa ambavyo wahusika wanaombwa kufika kuvitambua.