Masheha na Viongozi wa Serikali za Mitaa wameshauriwa kushirikiana na wananchi kujadili changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi ili kuzipatia ufumbuzi.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Jumuiya ya Mazingira na Utetezi wa Kijinsia Pemba PEGAO Ndugu Hafidh Abdi Said huko katika ofisi za Pegao Chake Chake, amesema ushirikishwaji wa wananchi katika kujadili changamoto zinazowakabili kutasaidia kwa kiasi kikubwa kupatiwa ufumbuzi kwa changamoto hizo.
Aidha Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa kupitia wahamasishaji jamii 39 kutoka Wilaya zote za Pemba jumla ya changamoto 44 zimeibuliwa mwaka 2022.
Kwa upande wake mratibu wa chama cha Waandishi wa habari wanawake Tanzania TAMWA upande wa Pemba Bi. Fat-hiya Mussa Said, amesema wamezishukuru taasisi mbali mbali za Serikali katika kufanikisha kutatua kero mbali mbali ambazo ziliibuliwa na wananchi katika mikutano yao.
Ameongeza kuwa miongoni mwa sababu zinazopelekea wanawake na vijana wengi kukosa haki ya kupatiwa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi pamoja na vyeti vya kuzaliwa ni pamoja na akina mama kukosa vizazi hai Kwa kujifungulia nyumbani bila ya kutoa taarifa kwa Masheha.
Alisema "Na ndio maana hata katika hili suala la watu kukosa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi na vyeti vya kuzaliwa tumegundua kuwa Kuna sababu nyingi ikiwemo kukosa vizazi hai inamaana kuwa Bado Kuna wazazi wanaendelea kujifungulia majumbani na wale watoto hawaandikishwi katika madaftari ya Shehia mwisho wa siku wale watoto wanakosa haki Yao yakupata vyeti vya kuzaliwa"
Nae Mtaribu wa mradi wa kuwajengea uwezo wanawake katika maswali ya Uongozi (SWIL) Dina Juma Makota, amesema uundwaji wa kamati za Shehia zimesaidia kwa asilimia 80 katika kuibua na kutatua kero za wananchi katika Shehia mbali mbali.
Alieleza "Kupitia uundwaji wa kamati katika Shehia mbali mbali ni jambo ambalo limesaidia Kwa asilimia 80% kutatua kero za wananchi katika Shehia mbali mbali hizi kamati zinaonekana Zina nguvu zenye ari na zenye malengo ya kutatua kero za wananchi kwahivyo uundwaji wa kamati za Shehia ni silaha kubwa za kuibua na kutatua changamoto za wananchi"
Mradi huo wa miaka minne wa kuwajengea uwezo wanawake katika masuala ya uongozi unaendeshwa na Chama cha waandishi wa Habari wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar, Chama cha wanasheria wanawake Zanzibar ZAFELA na Jumuiya ya Utetezi wa mazingira na jinsia Pemba PEGAO kwa kushirikiana na Ubalozi wa Norway.