Kufuatia kauli ya mbunge wa Makambako, Deo Sanga ya kuitaka Chadema kutosimamisha mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe amesema watasimamisha wagombea ngazi zote kwa kuwa bado wanapambana na CCM.
Sanga (CCM) alitoa ombi hilo kwa Chadema bungeni jijini Dodoma juzi wakati akichangia hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi kwa mwaka wa Fedha 2023/23, huku akisema Mbowe hawezi kukataa maombi yake.
“Ombi langu kwa Mbowe, kwa sababu anataka kuwafanyia maendeleo Watanzania na mama ameshafanya kazi kubwa dunia inamwelewa, 2025 Mbowe tulia mwachie mama.
“2025 Mbowe shiriki na wabunge, shiriki na madiwani, nafasi ya urais mwachie mama,” alisema.
Akizungumza jana kwa simu na Mwananchi, Mbowe alisema Chadema haipo kwa ajili ya kumbeba Rais Samia.
"Sipendi sana kucomment in person kuhusu Sanga, lakini Chadema haipo kwa ajili ya kumbeba Rais Samia, atabebwa na chama chake (CCM). Tutapambama na Chadema kitakuwa na wagombea wa urais wazuri sina wasiwasi na hilo.