Jeshi la Polisi mkoani Iringa linamshikilia Amani Martin (47) mkazi wa Nzihi mkoani humo kwa tuhuma za kumlawiti mtoto wake wa kumzaa mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi 10.
Akizungumza na waandishi wa habari Jumanne Aprili 11, 2023 Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani humo, ACP Allan Bukumbi amesema taarifa za ulawiti zilitolewa na mama mzazi wa mtoto huyo, Magret (29) Machi 28, 2023 baada ya kugundua tukio hilo.
Kamanda Bukumbi amesema kitendo hicho kimemsababishia maumivu makali katika sehemu za haja kubwa za mtoto huyo ambaye jina limehifadhiwa.
"Mbinu aliyotumia mtuhumiwa ni kumshika mtoto kwa nguvu na kumfanyia kitendo hicho cha kikatili wakati wakiwa shambani baada ya mama wa mtoto kuondoka kwenda kuokota kuni na kumuacha mtoto wake akiwa na baba yake", ameeleza Bukumbi.
Bukumbi amesema sababu za mtuhumiwa kufanya kitendo hicho alijitetea kuwa shetani alimpitia.
"Mtuhumiwa anajishughulisha na kazi ya uganga wa kienyeji, kiini cha tukio hilo bado kinachunguzwa, mtuhumiwa amekamatwa na taratibu za kisheria zinaendelea kuchukuliwa dhidi yake", amesema Kamanda Bukumbi.