Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata watuhumiwa wanne eneo la Kibugumo, Kigamboni wakiwa wanaiba mabomba ya mradi wa maji wa Kisarawe II kwenda Kigamboni.
Akiongea na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, SACP. Muliro J. Muliro amesema watuhumiwa hao wamekamatwa tarehe 08/04/2023 maeneo ya Kibugumo, Wilaya ya Kigamboni wakiwa na mabomba aina ya PVC inchi 6 wakiwa na gari yenye namba za usajili T. 719 AGL aina ya Mitsubish Canter.
Aidha SACP Muliro amesema "Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na wananchi limefanikiwa kumkamata dereva wa Canter aliyefahamika kwa jina la Emanuel Msofe mkazi wa Keko Magurumbasi na wenzake watatu wakiwa wanajianda kusafirisha mabomba hayo."
SACP. Muliro ameongeza kuwa, Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linafanya mahojiano ya kina na watuhumiwa hao ili kubaini kabla ya kuwakamata, wameiba mara ngapi mabomba hayo na mambomba mangapi yameshaibwa tayari.
Pia Kamanda Muliro amesema ufuatiliaji wa kina unafanyika kubaini mtandao wa wezi wa vifaa hivyo vya mradi wa maji ili kuona kama kuna watuhumiwa wengine wanahusika kuiba, kuuza au kuuziwa ili sheria ziweze kuchukuliwa haraka.
"Jeshi la Polisi halikubaliani na wizi huo na litafanya kila jitihada, kufuatilia kwa yeyote aliyehusika na wizi huo na hatua kali za kisheria zinachukulia ili kuona miradi ya serikali haichezewi" SACP Muliro alisema.
Mradi huo wa maji wa Kisarawe II ni miongoni mwa miradi mikubwa inayotekelezwa na serikali ya awamu ya sita inayosimamiwa na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kusambaza maji kwa wakazi wa Kigamboni.