Baraka Matamburo (30) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Mwanzo Kariakoo akikabiliwa na shitaka la wizi wa TSh 245,000, mali ya Grace Mwinuka.
Baraka alisomewa shitaka na karani, Emmy Mwansasu mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Kariakoo, Claudis Kipande.
Akisoma hati ya mashitaka, Emmy alidai mbele ya mahakama kuwa kijana huyo anashitakiwa kuiba Aprili 26, mwaka huu saa 10:30 jioni katika eneo la Hospitali ya Taifa Muhimbili, Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam ambaye ni mlinzi hapo.
Mshitakiwa alikana mashitaka hayo. Mlalamikaji, Grace aliieleza mahakama atakuwa na shahidi mmoja katika kesi hiyo. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 9, mwaka huu itakaporudi mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.
Mshitakiwa ataendelea kubaki rumande kwa kuwa ameshindwa kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na mdhamini mmoja atakayesaini bondi ya Sh 200,000.