Vitendo vya ushirikina na kupiga ramli chonganishi vimesababisha mkuu wa shule ya Sekondari Imenya Kata ya Itwangi Halmashauri ya Shinyanga Seleman Karavina kusimamishwa kazi kutokana na kupeleka mganga wa kienyeji shuleni na kupiga ramli chonganishi.
Akizungumza kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani cha robo ya tatu ya mwaka, Diwani wa Kata ya Itwangi Sonya Jilala alisema baadhi ya wanafunzi walikuwa wakianguka mapepo hovyo na kupiga kelele.
Alisema hali hiyo ilizuwa taharuki shuleni baada ya mwalimu kupeleka mganga wa kienyeji shuleni na kupiga ramli chonganishi ambayo iliwatuhumu baadhi ya wazazi wanahusika kufanya vitendo vya kishirikina na kusababisha taharuki.
“Haya mambo yametokea hivi karibuni ambapo mwanafunzi mmoja wa kidato cha pili aliandikiwa barua na watu wasiojulikana akituhumiwa yeye na wazazi wake ni washirikina watauawa” alisema Mhela.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Shinyanga Nice Munissy amekiri kupokea taarifa ya mwalimu huyo na tayari amemsimamisha kazi ili kupisha uchunguzi dhidi ya tuhuma zinazomkabili huku akiwaonya watumishi wengine wa umma kutojihusisha na vitendo hivyo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Johari Samizi amesema kitendo cha mwalimu mkuu kupeleka mganga wa kienyeji shuleni kimemsikitisha na kutaka apewe majibu ya kina na kuahidi kwenda kwenye shule hiyo